Changamoto zinatusaidia kujua umuhimu wetu nchini- Rais TEC

Na Pascal Mwanache, Mwanza
ASKOFU wa Jimbo Katoliki Mpanda ambaye pia ni Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) Mhashamu Gervas Nyaisonga amewataka wahitimu waliohitimu katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino Tanzania (SAUT) kukabiliana na changamoto mbalimbali watakazokutana nazo ambazo zitakuwa kinyume na matarajio yao, na kwamba changamoto zinasaidia kujua umuhimu wa mtu au taasisi.
Amesema hayo katika mahafali ya 20 ya SAUT yaliyofanyika katika viwanja vya Raila Odinga chuoni hapo Desemba 7, 2018, na kusema kuwa hata SAUT inakutana na changamoto ambazo ni kinyume na matarajio ya uanzishwaji wa chuo hicho miaka 20 iliyopita.
“Changamoto zinatusaidia kujua tuna nguvu kiasi gani, na kujiwekea viwango. Matarajio yenu yanaweza yasiwe sawa na mlivyotazamia. Ni sawa na Baraza la Maaskofu  lilipoanzisha vyuo hivi. Matarajio siyo kama tunavyoona. Chuo mama SAUT kinahitimu sasa mahafali ya 20. Kilikuwa na matarajio makubwa. Lakini mnajua kwamba tunapita katika kipindi chenye changamoto. Lakini tunazifurahia, kwani zinatusaidia kujua kuwa tuna umuhimu. Mtu ahangaiki na mtu mdogo. Changamoto zinatusaidia kujua tuna ukubwa kiasi gani. Zinatuhamasisha kutafuta focus ya uhakika” amesema Askofu Nyaisonga.
Aidha amewataka wahitimu hao waende wakaitumikie jamii kiaminifu kwa kuwa mstari wa mbele katika kutatua changamoto mbalimbali.
“Jamii inawategemea. Mjione kwamba ninyi ni wapambanaji, muwe mstari wa mbele. Kishawishi kikubwa katika dunia ya leo ni kuutafuta usalama wa sasa na kuacha usalama wa kesho. Tazama katika upana kesho yako. Hekima ni uwezo wa kuamua vizuri masuala yanayohusu maisha na mwenendo, malengo na mbinu zake. Ni matumizi sahihi ya maarifa ambamo ndani yake kuna elimu. Ni kinyume cha upumbavu” ameongeza.
Amewataka kujishikamanisha na hekima kimungu kwani hekima ya kidunia peke yake itawapotosha. Amesema kuwa kuna hatari ya kufikiri kuwa mtu amekamilika katika hekima kumbe tu amebaki katika hekima ya kidunia.
“Si haba ukakuta mtu na elimu yake yote akasema ipo ndoa ya jinsi moja. Akasimama na kuthubutu kusema kuwa hii ni haki kabisa. Hii ni hekima ya kidunia lakini imepungukiwa na hekima ya kimungu. Ziko nchi ambazo wanapeleka muswada wa kuhalalisha mambo haya. Ukiyapima unaona kuna upungufu mkubwa wa hekima. Mnahitimu nyakati hizi ambazo zinatambulishwa na kasi ya maendeleo, ugunduzi na mahusiano. Ni vizuri mjue kwamba mnaenda kwenye mapambano” amesema.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa Baraza la chuo cha SAUT ambaye pia ni Askofu wa Jimbo Katoliki Geita Mhashamu Flavian Kassala amewataka wahitimu hao wakawe afanyakazi mahsusi, wabunifu, wakarimu, wenye kuheshimu taratibu za kazi, kuheshimu utu na kuwajali binadamu wengine hasa wale walio wanyonge.
“Taifa linawaangalia na kuwategemea. Msisite kutumia ujuzi kusaidia na kuhakikisha taifa letu linajengwa na linasonga mbele na katika dira zinazowekwa katika nchi hususani dira ya viwanda” ameeleza.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU