Walei ni uhai wa Kanisa-Askofu Ruzoka

Na Thomas Mambo-Tabora
Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Tabora  Mhashamu Paul Ruzoka amewakumbusha walei kuchukua nafasi yao katika Kanisa bila kusahau wajibu wao wa kutakatifuza malimwengu bila kusita kwani ni wajibu wao.
Rai hiyo ameitoa hivi karibuni alipokuwa akitoa mahubiri yake katika kanisa la kiaskofu la Mtakatifu Terezia wa Mtoto Yesu Tabora na kuhimiza waaamini kukimbia dhambi na kuishi maisha yanayompendeza Mungu wakiwa bado hapa duniani.
Akitoa mahubiri yake Askofu Mkuu Ruzoka amesema Mtaguso wa Vaticano wa mwaka 1965 ulioweka wazi nafasi ya walei kuwa ni moja ya nguzo muhimu katika uhai wa Kanisa,”Walei ni wengi, wana nguvu na wanapatikana katika kila sehemu kama vile, mitaani, vijijini, vigangoni , maeneo ya kazi, na hata maeneo ya  biashara wakitumika vizuri wana nguvu kubwa ya kueneza Imani Katoliki,” Askofu Mkuu Ruzoka amesema.
Aidha amesisitiza umuhimu wa familia zote kuishi Imani Katoliki na kudumisha maadili katika ndoa zao  ili kupata mapadri na watawa wenye kupeleka sura ya Kristo Yesu kwa watu.
Pia amewaomba mapadri  kuonesha umuhimu wa huduma ya padri katika Kanisa, kwani bila mapari Imani Katoliki iko mashakani, na hivyo kutoa wito kwa mapadri wote kuhudumia waamini kwa moyo wa upendo na furaha.
Mapadri ndio wanao walisha watu Neno la Mungu na Sakramenti za Kanisa, hivyo wazazi wote hawana budi kulea miito mitakatifu katika famili zao.  Katika Adhimisho hilo la Misa Takatifu Jubilei ya miaka 50 tangu kuanzishwa kwa Idara ya Halmashauri walei ilizinduliwa.
Katika sherehe hiyo ya Familia kijimbo, madekano wa dekania zote tatu walitoa taarifa ya michango ya kutegemeza ofisi ya Askofu na kupokelewa.Aidha katika Misa hiyo, Askofu Mkuu Ruzoka aliwaalika waamini wote kumshukuru Mungu kwa kutimiza miaka 90 kijimbo tangu kupatikana kwa mapadre watatu wanajimbo, yaani Padre .Philipo Luziga, Padre Simoni Makulumo, na Padre Raphael Kavula ambao wote ni Marehemu.
Akimalizia mahubiri yake , Askofu Mkuu Ruzoka amewaalika mapadri, watawa na waamini wote kutolea sala zao na kumuombea aliyekuwa Askofu wa Jimbo Katoliki  Mbeya marehemu Askofu Evarist Chengula pumziko la milele.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU