Ask. Chengula mshumaa uliozima

 

Na Sarah Pelaji
Kanisa Katoliki Tanzania limepata pigo baada ya kuondokewa na Askofu wa Jimbo Katoliki Mbeya Mhashamu Evaristo Chengula  aliyefariki kwa ugonjwa wa moyo Novemba 21 mwaka huu katika hospitali ya  Moyo ya Jakaya Kikwete katika hospitali ya Taifa Muhimbili jijini Dar es Salaam alipokuwa anapata matibabu.
 Taarifa kutoka Ofisi ya Katibu Mkuu Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Padri.Dr. Charles Kitima zinasema kuwa, Marehemu Askofu Chengula ameaga dunia akiwa na umri wa miaka 77 ya kuzaliwa ambapo amezaliwa January I mwaka 1941.
Atazikwa Novemba 27 mwaka huu saa nne asubuhi katika Kanisa la Kiaskofu la Mtakatifu Antoni wa Padua Jimbo Katoliki Mbeya.
Akizungumza na Gazeti hili, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Mhashamu Gervas Nyaisonga amesema kuwa, Kanisa limepoteza Askofu mwenye fadhila mbalimbali ikiwemo ya uvumilivu, ucheshi, mpenda watu, mpole na msahimivu.
“Ninawapa pole Maaskofu wote wa Kanisa Katoliki kwa kuondokewa na mmoja wa wachungaji wakuu katika Kanisa la Tanzania.
Pia ninawapa pole wanakanisa wa Tanzania, Mapadri, watawa na walei wote hususani mapadri wa Jimbo Katoliki Mbeya, watawa wa kiume na kike, waamini waamini, viongozi mbalimbali wa dini na serikali jimboni Mbeya.
Ninawaasa tuiombee roho ya marehemu iweze kupokelewa Mbinguni na kupokea msiba huu kwa imani tukijua kuwa, sisi wakristo njia yetu ya kwenda kwa Baba ni kifo, ni katika kufa ndipo tunapata uzima wa milele,” amesema Askofu Nyaisonga.
Aidha amesema kuwa Marehemu Askofu Chengula alikuwa baba mwema, mpenda watu na mcheshi ndiyo maana hata picha zake zinazosambaa kwenye mitandao anaonekana anatabasamu kwa sura ya upendo.
Ni mtumishi mwaminifu mwenye busara ambaye amefanya kazi ya kulitumikia Kanisa la Mungu kwa uaminifu, amemaliza mwendo, amemaliza kazi yake maana katika umri alionao amefanya mengi.
“Sisi mapadri wa jimbo lake la Mbeya tulifurahia na kuridhishwa na utendaji kazi wake kwani alikuwa baba anayeendeleza maisha ya mapadri, wengi tulijiendeleza kielimu katika fani mbalimbali na amekubali kututoa kufanya kazi katika taasisi za Kanisa .
Hiyo inaonesha moyo wake wa kujitolea kwa Kanisa. Kuna mapadri wanafanya kazi AMECEA, Walimu katika vyuo vikuu, Baraza la Maaskofu, kuna mapadri madaktari wa binadamu na fani mbalimbali. Hayo yote ni matunda ya kazi yake,” amesema.
Amewataka waamini, mapadri na Kanisa kwa ujumla kuendelea kumuenzi husuani katika fadhila ya upole, uvumilivu, upendo, uthubutu, ukarimu na ucheshi ili kujenga jumuiya yenye amani na furaha.
Katibu mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania amesema Padri Dr. Charles Kitima ameeleza kuwa, Marehemu Askofu Chengula aliwasili Jijini Dar es Salaam, Novemba 20 mwaka huu akiwa anasumbuliwa na ugonjwa wa moyo.
Alipelekwa kwenye Taasisi ya Moyo ya Jakaya Kikwete katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili, na kulazwa ili aendelee na matibabu.
 Jitihada za Madaktari kutaka kuokoa maisha yake, hazikufanikiwa ndipo  majira ya saa tatu asubuhi ya Novemba 21 mwaka huu aliaga dunia.
Baadhi ya wanaharakati wa uhai (Pro-life) wamesema kuwa Askofu Chengula ameacha alama katika taifa hili kwani ni hivi karibuni tu amewataka wananchi na serikali kukemea na kupinga ushoga kwa nguvu zote.
Ikumbukwe kuwa, wiki moja iliyopita Marehemu Askofu Chengula alisikika sana kwenye vyombo vya habari Tanzania huku akipongezwa kauli yake aliyosema kuwa Ushoga ni ushetani.
Kuhusu suala la Ushoga Askofu Chengula alisema kuwa licha  ya  Vitabu Vitakatifu kuelezea kuwa ushoga ni  dhambi pia siyo utamaduni wa watanzania.
 Hivyo aliwataka watanzania kuwa makini  na watu wasiolitakia taifa mema na wanaotaka kuliingiza Taifa katika matendo maovu ya aibu yasiyompendeza Mungu.
“Hawa watu wa haki  za binadamu wajikite katika masuala ya kupiga vita utoaji  wa mimba na kuuwa watoto  wasio na hatia na siyo mambo ya ushoga, ni dhambi kubwa.
Nimependezwa sana na kauli ya ya huyu Waziri  wa mambo ya ndani alipoonyesha msimamo  bungeni kuwa Tanzania ni hekalu la Roho Mtakatifu na hivi haipaswi kuchezewa chezewa kwa vitendo   visivyompendeza Mungu  ukiwemo ushoga,”alisema enzi za uhai wake wiki moja iliyopita.
Kwa wanachuo wote Askofu Chengula aliwapa wosia wa kuzingatia taaluma akiwakataza kujiingiza kwenye siasa.
Alisema Kanisa lingependa kuona  wahitimu watakaomaliza wanaopata elimu katika vyuo vya Kanisa ni wahudumu wa jamii wanaotoa huduma wakizingatia weledi na haki bila ubaguzi wa  itikadi zao vya vyama wala imani za dini zao.
“Hatutavumilia wanafunzi wanaojihusisha na siasa kwa kutumiwa na vyama vya siasa kuingiza masuala hayo  vyuoni hasa vyuo vya Kanisa  hali ambayo inaweza kuleta mgawanyiko miongoni mwa wanafunzi. Someni kwanza mkimaliza ndipo mshikamane na mambo mengine nje ya taaluma.
Lengo la wanafunzi kwenda shule ama vyuo vya Kanisa ni kuwajengea uelewa, kuwaimarisha  na kuwaendeleza watanzania kitaaluma wapate maarifa waweze kulitumia Taifa . Siasa ni nje ya lengo na zinawapotezea muda.
Tusingependa  kuona wala kusikia  wanafunzi wakijihusisha na CCM, Chadema, Cuf na vyama vingine vyovyote. Nasema siasa ni marufuku,” amesema wiki moja iliyopita akiwa hai huko SAUT Mbeya.
Alitahadharisha juu ua uchaguzi unaokuja ambapo siku ya Injumaa Kuu mwaka huu aliwaasa  waamini na wananchi kuchagua viongozi sahihi na watakaokidhi mahitaji yao badala ya kufanya makosa kwa kuchagua viongozi wasiofaa na kuanza kulalamika baada ya uchaguzi.
Amesema imekuwa ni kawaida kwa maaskofu na wadau wengine kuanza kukosoa viongozi baada ya uchaguzi, jambo ambalo halina faida sana, na hivyo wao kama maaskofu mwaka huu wameamua kuwataka waumini wao kuwapima kwa umakini watu wote watakaojitokeza kugombea nafasi mbalimbali za uongozi katika chaguzi zijazo kwa kuanzia na uchaguzi wa serikali za mitaa utakaofanyika mwakani.

 Wasifu mfupi wa marehemu
Askofu Evaristo Marcus Chengula alizaliwa tarehe Mosi Januari 1941, huko Mdabulo, Wilaya ya Mufindi, Mkoani Iringa. Baada ya masomo ya utawa na upadri, Oktoba 15 mwaka 1970 alipewa Daraja Takatifu ya Upadri.
Novemba 8 mwaka 1996, Mtakatifu Yohane Paulo II alimteuwa kuwa Askofu wa Jimbo Katoliki Mbeya na kuwekwa wakfu kama Askofu Februari 2 mwaka 1997.
Amefariki dunia akiwa amelitumikia Kanisa kama Padri kwa muda wa miaka 48 na Askofu kwa muda wa miaka 21.
Raha ya milele umpe ee Bwana na Mwanga wa milele umwangazie apumzike kwa amani, Amina.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU