Heri tufe kwa njaa kuliko misaada yenye shinikizo la ushoga-Kard. Pengo

Na Philipo Josephat - Dsm
ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki  Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amepongeza na kufurahia msimamo wa serikali dhidi ya kauli ya baadhi ya mataifa ya Magharibi kutishia kusitisha misaada kwa Tanzania kwa kuwa nchi inapinga ushoga.
Ametoa msimamo huo hivi karibuni katika maadhimisho ya Misa Takatifu ya Mavuno iliyofanyika kijimbo katika Viwanja vya Msimbazi Centre, vilivyopo Jimbo Kuu Katoliki  Dar es Salaam.
Kardinali Pengo amesema kuwa yapo baaadhi ya mataifa yanayotishia kukata misaada kwa nchi zinazopinga ushoga na mahusiano ya watu wa jinsia moja hivyo Kardinali Pengo amesisitiza kuwa, ni heri kufa kwa njaa kuliko kupokea misaada yenye shinikizo la kufanya mambo machafu yaliyo kinyume na Mungu.
Kiongozi huyo wa kiroho amesema kuwa, uchafu wa mahusiano ya watu wa jinsia moja ndio uliosababisha Sodoma na Gomora kuangamizwa na kwamba, mambo hayo ni kinyume na mpango wa Mungu katika uumbaji, hivyo hayawezi kukubalilika.
“Tunaishukuru Serikali kwa msimamo wake kuhusu jambo hili, na sisi kama Watanzania hatuwezi kuyakubali mambo hayo yasiyompendeza Mungu; na kama ni kufa na njaa basi tufe na Mungu wetu,” amesema Kardinali.
“Tunalolifanya  tunasema kitu kimoja kwa Mungu kwamba, kama tutakufa kwa njaa  tutakufa na wewe, kama wanataka tuwe na ndege zisizo na marubani katika mambo machafu, basi sisi tutabaki na wewe na si ndege wala magari ya kifahari, kwa sababu kumpuuza Mwenyezi Mungu ni kujipuuza wenyewe,” amesema Kadinali Pengo.
Ikumbukwe kuwa hivi karibuni, Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Kangi Lugola, alisema kamwe vitendo vya ushoga haviruhusiwi na kila kiungo kilichoumbwa na Mungu katika mwili wa mwanadamu kina kazi yake hivyo, Serikali ya Tanzania haitakubali vibadilishiwe matumizi.
Waziri Lugola alitoa kauli bungeni Dodoma baada ya Mbunge wa Konde, Khatibu Saidi Haji, kutaka msimamo wa Serikali kuhusu vitendo vya ushoga.
Akasema: “Serikali yetu kamwe haitaruhusu mwanadamu yeyote kubadili matumizi ya kiungo ambacho kimekusudiwa kwa ajili ya kutolea haja, kitumike katika matumizi mengine ambayo Mungu hakuyakusudia.”
Kauli hiyo imeridhisha Maaskofu wa Kanisa Katoliki na Mwadhama Kardinali Pengo ambaye anakuwa Askofu wa pili kupinga ushoga hadharani huku Marehemu Askofu Evaristo Chengula aliyekuwa Askofu wa Jimbo Katoliki  Mbeya akiwa wa kwanza kupinga vitendo vya ushoga hadharani siku kadhaa kabla hajafikwa na mauti.
Pia katika Ibada ya Misa Takatifu ya  kumwaga Marehemu Askofu Chengula iliyofanyika Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) Kurasini Dar es Salaam Novemba 29 mwaka huu kabla ya kusafirishwa kwenda Mbeya kwa maziko, Rais John Magufuli alimtaja Mhashamu Chengula kama mtu wa Mungu aliyekemea ushoga hadharani.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU