Askofu Kinyaiya aonya vijana kuhusu mavazi yenye tamaduni za nje

Na Rodrick Minja, Dodoma.
Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dodoma Mhashamu Beatus Kinyaiya amewataka vijana kuvaa mavazi yanayositiri miili yao wakizingatia tamaduni za kiafrika na imani yao.
Askofu Mkuu Kinyaiya amesema hayo hivi karibuni katika Parokia ya  Mtakatifu Petro Swaswa jimboni humo alipokuwa anatoa Sakramenti ya Kipaimara kwa vijana 75 na kuzindua duka la Jimbo la kuuza visakaramenti vya Kanisa.
Amewataka vijana walioimarishwa kwa sakramenti hiyo kutokuiga tamaduni ambazo zinaaibisha utu wao na imani yao hasa mavazi kwani sio kila tamaduni inapaswa kuigwa.
“Vijana ninawaombeni tena sana msikubali kufuata tamaduni ambazo zinakwenda kinyume na maadili yetu ya kitanzania fuateni tamaduni zetu zenye maadili ,” amesema Askofu Mkuu Kinyaiya
Kwa upande wa suala la Utandawazi Askofu Mkuu Kinyaiya pia amewataka vijana kuwa  makini katika suala la utandawazi maana hilo ndilo linalowasababisha watu kuacha tamaduni zao na kuanza kuishi tamaduni za kigeni ambazo matokeo yake yanakuwa sio mazuri katika jamii.
Sambamba na hayo pia amewakumbusha wakristo wote kukataa kuyumbishwa kiimani na kitamaduni kwani karne ya sasa ina makelele na sauti nyingi. Kuzitambua zauti zilizo sahihi kunahitahi hekima na werevu.
 Aidha  amelipandisha hadhi na kuzindua duka la visakramenti la Parokia kuwa la jimbo lililogharimu zaidi ya shilingi milioni 30.2.
Akitoa taarifa ya  ujenzi wa duka hilo la visakramenti Paroko wa Parokia ya Mtakatifu Petro Swaswa  Padri Antipas Shayo amesema kuwa duka hilo linategemea kuuza bidhaa mbalimbali kulingana na imani ya Kanisa Katoliki, na bidhaa hizo ni pamoja na vitabu, rozari, vitenge vya wawata, Pete, misalaba, sanamu na vinginevyo vyenye nia ya kuueneza ukristo.
Padri Shayo amesema duka hilo litaendeshwa na Halmashauri ya walei kwa niaba ya waamini chini ya usimamizi wa Paroko ambapo kiasi cha fedha kitakachopatikana kitawezesha waamini kuhudumiwa huduma mbalimbali za kiimani na kijamii.
Hata hivyo amesema kuwa kamati ya fedha, uchumi na mipango itahusika na utendaji wa shughuli za kila siku na itawajibika kufahamu kiasi cha mali kilichoingizwa na kupokelewa kwenye vitabu.
Aidha Padri Shayo amesema mpango wa baadae wa Parokia hiyo ni kujipanga na kuhakikisha kuwa mafundisho ya dini yanapewa kipaumbele katika jumuiya, shuleni na nyumbani.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU