Serikali yashangazwa na uwezo wa Chuo Kikuu cha Mt. Yosefu


Na Pascal Mwanache, Dar
MAONESHO ya miradi bunifu ya wanafunzi wa Chuo Kikuu cha Mtakatifu Yosefu Tanzania, wa Uhandisi, Ualimu wa Sayansi na Hisabati, na Udaktari wa Binadamu yanayofanyika Agosti 29 hadi 31, 2018 ndani ya viwanja vya Mlimani City yameifanya serikali ikiri kuwa kiwango kikubwa cha elimu inayotolewa na chuo hicho itasaidia kutatua changamoto mbalimbali katika jamii.
Hayo yamesemwa na Naibu Waziri, Sera, Bunge, Kazi, Vijana, Ajira na Walemavu, Anthony Mavunde  ambaye alikuwa mgeni rasmi katika uzinduzi wa maonesho hayo, na kusema kuwa vijana hao watasaidia kukuza falsafa ya serikali ya awamu ya tano ya Tanzania ya viwanda.
“Kwanza kabisa nataka nikiri kwamba leo ndio nimeona kwa kiwango kikubwa elimu inayokwenda kumsaidia mtanzania kutatua matatizo mbalimbali katika jamii.  Nimefurahi sana kuwaona vijana wa kitanzania wanachuo wakionyesha uwezo wa juu kabisa kuja na utatuzi mbalimbali wa matatizo tuliyonayo na namna bora ya kuweza kuyakabili matatizo hayo” amesema.
Aidha ameeleza kuwa maonesho hayo yanampa ujasiri kwamba nchi itapiga hatua kubwa ya maendeleo kwa kuwatumia wataalamu wa ndani, kikubwa wanachohitaji ni uwezeshwaji.
“Huwa najisikia vibaya sana kusikia tunawasifia vijana wa nchi jirani kwamba wana uwezo mkubwa. Vijana wa kitanzania mna uwezo mkubwa sana wa kwenda kushiriki kwenye ustawi wa Taifa letu na kuikuza Tanzania hasa katika falsafa ya serikali ya awamu ya tano ya serikali ya viwanda. Pongezi kwa Chuo cha Mtakatifu Yosefu, nilikuwa napita pale barabarani nakiona lakini sikujua kama mko organized kwa namna niliyoiona leo” ameongeza.
Pia Mavunde amebainisha kuwa ubunifu huo ni namna kubwa ya kuunga mkono juhudi za serikali ya awamu ya tano ya serikali ya viwanda, kwa kuwaanda wataalamu ambao watasaidia nchi kupiga hatua.
“Kazi kubwa za kiubunifu zinakwenda kutatua changamoto mbalimbali. Kama nchi tukitumia wataalamu hawa wa ndani tutapunguza gharama za uendeshaji. Tukiwatumia vizuri wataalamu wetu wa ndani Taifa litapiga hatua mara dufu. Nimeona mifumo mbalimbali hapa kama ile ya kupunguza ajali, kilimo, ukusanyaji wa mapato nk” ameeleza.
Katika hatua nyingine Mavunde amevutiwa na ubunifu wa msichana mmoja ambaye amebuni teknolojia rahisi inayosaidia katika uhifadhi wa mafaili, na kuahidi kumpeleka binti huyo kwa waziri anayeshugulikia masuala ya Utumishi wa Umma.
“Moja kati ya changamoto tuliyonayo katika mifumo yetu ni pamoja na mfumo wa handling ya mafaili. Mengi hupotea, utafutaji wake hufanywa manually na huchukua muda mrefu, lakini leo kupitia wanachuo hawa wanakuja na suluhisho ambalo halina gharama kubwa. Na kama nilivyoahidi nataka nimchukue yule binti nimpeleke kwa waziri wa Utumishi  Mheshimiwa Mkuchika akae kwa dakika chache tu amsikilize alichonacho” amebainisha.
Kwa upande wake Makamu Mkuu wa Chuo hicho Prof. Burton Mwamila amesema kuwa wanafunzi wanaohitimu chuoni hapo wana uwezo mzuri wa kuweza kuchangia katika ajenda ya Tanzania ya viwanda, kinachohitajika ni mazingira wezeshi ili ule ubunifu wanaouonyesha wakiwa chuoni uweze kuendelezwa.
“Tuweke mikakati ya kuwawezesha hawa vijana kwa kuwa miradi mingi bunifu iliyoonyeshwa hapa inaweza ikageuzwa ikawa viwanda” amesema.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU