Msimamo wa Magufuli kuhusu uzazi wa mpango wapongezwa

Na Pascal Mwanache, Dar
MSIMAMO alioutoa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Dkt. John Pombe Magufuli juu ya uzazi wa mpango umepongezwa kwa kuwa kukithiri kwa vitendo vya matumizi ya vidhibiti mimba kumeharibu taifa na kushambulia maadili, utamaduni na imani ya taifa huku dhana hizo zikiwa ni itikadi ovu za magharibi za kudhibiti ukuaji wa idadi ya watu.
Pongezi hizo zimetolewa na Mkurugenzi wa Shirika la Kutetea Uhai nchini (Pro life) Emil Hagamu katika tathmini yake ambapo amesema kuwa watu wa Ulaya wamepita katika miongo mbalimbali, imefikia mahali wameharibikiwa hivyo mawazo na itikadi zao ovu ndizo zinazoletwa kwetu Afrika hasa Tanzania.
“Hiki ndicho Nyerere alichosema, alisema ili tuendelee tunahitaji watu, ardhi, siasa safi na uongozi bora. Kwa hiyo watu ndiyo namba moja. Asikudanganye mtu, nchi zote za Ulaya zilipata maendeleo kwa sababu kuu tatu: Walitunyonya kiuchumi na kisiasa, biashara ya utumwa ambapo walihitaji watu, na idadi yao ni kubwa. Uki promote contraceptives na abortion utasababisha idadi ya watu kupungua, na ikipungua kila kitu kinarudi nyuma” ameeleza Hagamu.
Aidha Hagamu ameweka wazi kuwa watu wa magharibi wanaokuja kuhamasisha matumizi ya vidhibiti mimba wanakabiliwa na upungufu wa idadi ya watu katika nchi zao ambako kwa sasa  wanahamasisha watu kuzaa na wamefungua milango kwa wahamiaji ili idadi ya watu isipungue sana.
“Tunamuunga mkono Rais na tunampa hongera na tunaomba aseme zaidi kwa sababu hawa mabeberu wanaotaka kutumaliza hawana nia njema. Sasa hawa kule kwao wanahamasisha kuzaa halafu wanakuja huku kwetu wanakuja kupunguza vizazi sasa huoni huu ni uendawazimu?” amehoji.

Msimamo wa Rais Magufuli
Akizungumza na wanachi wa Wilaya ya Meatu mkoani Simiyu katika mkutano wa hadhara, Rais Magufuli amesema kuwa hakubaliani na kampeni za uzazi wa mpango na kuwataka wanachi wafanye kazi na wakiwa na chakula cha kutosha wazae ili nguvu kazi ya taifa iimarike.
“Najua waziri hapa anapenda kuzungumzia uzazi wa mpango, na ndio maana mimi mambo mengine huwa sikubaliani nao. Ziko nchi zilipangiwa mpango wa kuzaa leo wanajuta wanatafuta mtu wa kuzaa katika nchi zao. Mimi nawaeleza ukweli, mtadanganyika kwa mipango mingine ya ajabu sana. Tunachotakiwa watanzania tuko milioni 55 ni kuchapa kazi ili kusudi utakaowazaa uwalishe. Kama huwezi kufanya kazi hapo ndipo uende kwenye mipango ya uzazi” ameeleza Rais Magufuli.
Aidha Rais Magufuli ameongeza kuwa “Mimi ninachowaomba ndugu zangu mbele ya Waziri wa Afya ambaye anaongea mambo ya ku control uzazi, limeni, fanyeni kazi, ukiwa na chakula cha kutosha zaa. Watu wameshaingiwa na mawazo ya ajabu katika nchi”.

Kanisa linasemaje?
Mwaka 1968, Baba Mtakatifu Paulo VI aliandika insiklika iitwayo ‘Humanae Vitae’  ikijibu kiu ya watu ndani ya kanisa, mintarafu matumizi ya vidhibiti mimba, kama ni vyema ama si vyema kutumia vidhibiti mimba, na kuainisha njia bora za kupanga uzazi kwa njia ya maumbile kama Mungu alivyoratibisha.
Hata hivyo ikumbukwe kuwa mnamo mwaka 1930, Umoja wa Makanisa ya Kianglikana katika mkutano wao wa Lamberth, ingawa walikubali kuwa, njia bora ya kupanga uzazi ni ile itumiayo mwenendo wa maumbile, lakini waliruhusu matumizi ya vidhibiti mimba kwa wanandoa wenye matatizo ya pekee.
Ruhusa hii ilifungua milango kwa matumizi ya vidhibiti mimba hata pasipo matatizo yoyote, na hatimaye ukawa ndio mtindo wa kupanga uzazi kwa watu wa ndoa.
Kutokana na ruhusa hiyo ya Waanglikana na kutokana na kuongezeka kwa vitisho dhidi ya taasisi ya ndoa, Baba Mtakatifu Pius XI, mnamo Decemba 31, 1930 alitoa tamko la Kanisa Katoliki kuhusu matumizi ya vidhibiti mimba.
“Kwa sababu yoyote, hata kama ni kubwa kiasi gani, haitaruhusiwa matumizi ya njia ambazo kwa asili yake ni ovu dhidi ya maumbile na kuzifanya zikubalike kimaadili kama vile zingekuwa njema. Kwa vile tendo la ndoa limeelekezwa kimaumbile katika uzao wa watoto, wale wanaoliharibu kwa makusudi na kuliondolea uwezo wake wanatenda dhambi dhidi ya maumbile na wanajiletea aibu na uovu wa ndani. (Casti Cannubii, Na 54)”


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU