Ask. Ngalalekumtwa aadhimisha Yubilei miaka 25 na kupadrisha mashemasi 13

Na Getrude Madembwe, Iringa
ASKOFU wa Jimbo Katoliki Iringa Mhashamu Tarcisius Ngalalekumtwa hivi karibuni ameadhimisha Yubilei ya miaka 25 ya uchungaji jimboni Iringa na katika maadhimisho hayo ametoa Daraja Takatifu ya Upadri kwa mashemasi 13.
Maadhimisho hayo yamefanyika katika viwanja vya kichangani na mara ya kwanza kwa jimbo hilo kupata idiadi kubwa ya  mashemasi na hivyo kuliweka katika historia.
Misa Takatifu ambayo imeongozwa na Askofu Mkuu Damian Dallu wa Jimbo Kuu Katoliki Songea na homilia kutolewa na Askofu Ngalalekumtwa imehudhuriwa na zaidi ya mapadri 100 kutoka ndani na nje ya jimbo la Iringa, watawa wa kike na kiume pamoja waamini kutoka sehemu mbalimbali za jimbo la Iringa
Akitoa homilia kwenye maadhimisho hayo, Askofu Ngalalekumtwa amewataka mapadri hao wapya wawe faraja, sala, huruma wapole wema na pia wawe waaminifu kwa viapo vyao.
“Jitahidini kuishi maisha ya kiinjili yaani ya baraka ili watu wampate Kristo ndani yao na pia waiendeleze kazi ya uinjilishaji, watambue kwamba wazazi wao wamewatoa kwa kanisa na kamwe wasirudi nyuma na wajue kwamba wao ni wajumbe wa habari njema” amesema.
 Awali kabla ya kuanza kwa misa hiyo Takatifu, Makamu wa Askofu Jimbo la Iringa Padri Vincet Mwagala ambaye pia ni Paroko wa Parokia ya Ifunda, amesema kwamba wanamshukuru Mungu kwa sababu miaka 25 iliyopita wana Iringa walipewa zawadi ya Kuhani, Mchungaji Mkuu wa Jimbo, Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa.
“Tunakushukuru wewe mwenyewe kwa kutii sauti ya Mungu, na hivi kututumikia kwa miaka hii 25, tunakuombea ili Mwenyezi Mungu aendelee kukujalia afya njema ya mwili na Roho. Baba, wewe umekuwa mtumishi wa wote, ndiyo maana leo tupo hapa wakristo na wasio wakristo kumtukuza Mungu kwa upendo wake ambao umekuwa ukidhihirika kupitia wewe mtumishi wake” amesema.
Kwa mujibu wa taarifa iliyoandikwa na Padri Marko Kihwelo kwa niaba ya kamati ya Liturujia Jimbo, imesema kuwa tarehe 06.01.1988 Baba Mtakatifu Yohane Paulo II, alimteua Padri Tarcisius Ngalalekumtwa kuwa Askofu Mwandamizi wa Jimbo la Sumbawanga ambako alijitoa mhanga katika kulitumikia taifa la Mungu kwa juhudi.
Askofu Ngalalekumtwa alihamishwa na Baba Mtakatifu Yohane Paulo II kutoka jimbo la Sumbawanga na kuwa askofu wa Iringa na tarehe 10.01.1993 alisimikwa rasmi kuwa Askofu wa jimbo la Iringa kushika nafasi ya Askofu Norbert Mtega ambaye alihamishiwa kuwa Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu la Songea.
Tangu kuingia kwake jimboni Iringa, parokia kadhaa zimeongezwa ambazo ni Migoli, Mtandika, Madege, Nyololo, Ipogolo, Kidamali, Parokiaya vyuo vikuu, Mapanda na Mbarali, mpaka sasa Jimbo la Iringa lina jumla ya parokia 38.
Askofu Tarcisius Ngalalekumtwa alizaliwa tarehe 25.10.1948 katika kijiji cha Banavanu Parokia ya Tosamaganga Mkoa wa Iringa kwa wazazi Joseph Ngalalekumtwa na Mama Magdalena Sekutika. Alibatizwa Parokiani Tosamaganga tarehe 15.11.1956 na kupewa sakramenti ya kipaimara siku hiyo hiyo na mhashamu Askofu Attilio Beltramino, I.M.C, na komumyo ya kwanza.
 Mwaka 1956 alianza masomo ya elimu ya msingi katika shule ya msingi wavulana Tosamaganga ambayo kwa sasa inaitwa shule ya msingi Lupalama A hadi mwaka 1959. Mwaka uliofuta alijiunga na seminari ndogo ya Tosamaganga ambapo alisoma hadi mwaka 1967. Akiwa  na wito wa kumtumikia Mungu katika upadri, aliamua kuendelea na masomo ya seminari, mwaka 1968 alitumwa seminarini Kuu ya Peramiho kujiunga na masomo ya Falsafa.
 Mwaka 1969 alitumwa Roma, Italia, kusomea Teolojia katika Chuo Kikuu cha Propaganda Fide. Alisoma chuoni hapo hadi  mwaka 1974 alipohitimu masomo yake vizuri na kujipatia shahada katika fani ya Elimu Mungu ( Lincence in Dogmatics). Tarehe 07/04/1973 alipata Daraja Takatifu ya Upadri huko San Ginesio, Camerino, Italia alipewa na Askofu Bruno Frattegiani.
Akiwa padri tayari alirudi nchini Tanzania Oktoba 1974. Askofu Mario Mgulunde alimtuma Padri Ngalalekumtwa parokini Ifunda, huko alifanya utume kuanzia tarehe 18/11/1974 hadi tarehe 05/12/1976.
Mwaka 1977 alitumwa na Askofu Mario Mgulunde Seminari Kuu Peramiho kuwa mkufunzi na mlezi, kwa unyenyekevu alipokea utume huo. Haukupita muda mrefu, akateuliwa kuwa Gombera wa Seminari kuu ya Paremiho, akishika nafasi iliyoachwa wazi na mtangulizi wake Padri Emmanueli Mapunda, ambaye alitumwa Roma kwa masomo. Padri Ngalalekumtwa aliongoza seminari hiyo hadi tarehe 30.03.1982. bTarehe 11.04.1982, alitumwa seminari ndogo ya Mafinga kuwa Gombera hadi Desemba 1988.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU