Kanisa laondokewa na watumishi watano ndani ya siku 7

Na Pascal Mwanache na Antony Chilumba
KANISA Katoliki nchini limepata pigo mara baada ya kuondokewa na watumishi wake watano ndani ya siku saba, akiwemo Askofu Mstaafu wa Jimbo Katoliki Bukoba Mhashamu Nestor Timanywa, mapadri watatu na sista.
Taarifa iliyotolewa na Askofu wa Jimbo Katoliki Bukoba Mhashamu Desderius Rwoma na kuthibitishwa na taarifa kutoka Ofisi ya Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) inaeleza kuwa Askofu Nestor Timanywa amefariki Agosti 28, 2018 saa tano asubuhi katika Hospitali ya Rufaa Bugando jijini Mwanza alikokuwa amelazwa.
“Marehemu Askofu Timanywa amekuwa akisumbuliwa na saratani. Amepatiwa matibabu katika hospitali mbalimbali na mauti yamemfika akiwa katika Hospitali ya Bugando Mwanza. Baba Askofu Timanywa ameaga dunia akiwa na umri wa miaka 81 ya kuzaliwa, 51 ya upadri na 44 ya uaskofu” imeeleza taarifa hiyo.
Mazishi ya marehemu Askofu Timanywa yanafanyika Agosti 31, 2018 sa tano asubuhi katika Kanisa Kuu la Bikira Maria Mama mwenye Huruma, Jimbo Katoliki Bukoba.
Askofu Timanywa alizaliwa Mei 7, 1937 katika kijiji cha Kakungiri Parokia yaMugana Bukoba. Alipewa Daraja Takatifu ya Upadri Desemba 11 1966 na Mwadhama Laurean Kardinali Rugambwa. Novemba 26 1973 alitangazwa na Baba Mtakatifu Paulo VI kuwa Askofu wa Jimbo la Bukoba na akasimikwa Februari 24, 1974. Ameliongoza jimbo la Bukoba kwa zaidi ya miaka 39 hadi alipostaafu Januari 15 2013.

Padri Christian Mhagama
Mnamo Agosti 21 Askofu wa Jimbo Katoliki Mbinga Mhashamu John Ndimbo alitangaza kifo cha Padri Christian Mhagama, ambacho kilitokea saa kumi alfajiri katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili.
Mazishi ya marehemu Padri Mhagama yamefanyika Agosti  28, 2018 katika Makaburi ya Mapadri Kigonsera Jimboni Mbinga, na kuongozwa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Songea Mhashamu Damian Dallu na Askofu wa Jimbo Katoliki Mbinga Mhashamu John Ndimbo.
Marehemu Padri Mhagama atakumbukwa na wengi hasa alivyosikika pale alipokuwa mwandaaji na msimamizi wa Kipindi cha ujumbe wa Biblia kupitia Radio Maria Tanzania.
Akimuelezea Padri Mhagama, Askofu Ndimbo amesema kuwa watu wamefika kwa wingi kanisani kumuaga kwa sababu ameacha alama kupitia upendo wake na mafundisho aliyoyatoa kupitia vipawa alivyopewa na Mungu bila uchoyo unaosababishwa na ubinafsi.
Katika homilia yake Askofu Ndimbo amewaasa waamini kama wanadamu wanaosafiri hapa duniani, kutoishi maisha ya ubinafsi ambayo ameyataja kuwa chanzo cha mwanadamu kujitenga na Mungu.

Padri Genesius Kaiza
Mnamo Agosti 23, 2018 Askofu wa Jimbo Katoliki Rulenge Ngara Mhashamu Severine Niwemugizi alitangaza kifo cha Padri Genesius Kaiza kilichotokea Alfajiri Agosti 23 saa 10:30 maeneo ya Buseresere akiwa anapelekwa Hospitali ya Bugando.

Mazishi ya marehemu Padri Kaiza yamefanyika Agosti 25, 2018 yakitanguliwa na
Ibada ya Misa Takatifu iliyofanyika katika Kanisa la Kristo Mfalme Rulenge.
Akitoa homilia katika Misa hiyo Askofu Niwemugizi amesema kuwa imani katika ufufuko ndiyo sababu inayolisukuma Kanisa kuwaombea marehemu. Amesema kuwa uwepo wa ufufuko ndiyo sababu ya matumaini ya mkristo mkatoliki.

Padri Ernest Mangwinda
Askofu wa Jimbo Katoliki Lindi Mhashamu Bruno Ngonyani amewahimiza wanajimbo hilo kuzidi kumuomba Mungu ili vijana wengi waitikie wito wa kuwa mapadri na watawa kusudi waendeleze gurudumu la uinjilishaji.
Wito huo ameutoa Agosti 29, 2018 wakati akitoa homilia kwenye adhimisho la Misa ya Mazishi ya Padri Ernest Mangwinda(65) yaliyofanyika katika eneo la kuzikia mapadri wa Jimbo hilo lililoko Parokiani Nyangao.
Amesema kuwa kifo cha ghafla cha Padri huyo si tu kimeacha pengo la wachungaji katika Jimbo hilo, bali pia kinaongeza mzigo mzito wa kazi ya uchungaji ambayo inawaelemea mapadri wachache waliobakia katika huduma, mazingira ambayo amewataka waumini wa Lindi kuombea miito ili wapatikane mapadri wa kutosha.
Askofu Ngonyani amewaambia waombolezaji walioshiriki adhimisho hilo kuwa, hali ya miito katika Jimbo hilo na hata majimbo jirani ya Mtwara na Tunduru-Masasi hairidhishi hivyo umuhimu wa kuiombea miito ni mkubwa siku zetu hizi.
Akizungumzia kifo cha Padri Mangwinda, amesema kuwa ni cha ghafla, hali ambayo inamdai kila mtu kukesha au kuwa tayari muda wote kwa ajili ya kukutana na Muumba wake kupitia kifo.
Kwa upande wake Askofu James Almasi wa Kanisa la Anglikana Masasi, ambaye alihudhuria mazishi hayo aliunga mkono “kilio” cha Askofu Ngonyani kwa kuwakumbusha wakristo kwenye majimbo ya Lindi, Mtwara na Tunduru Masasi, wajibu walionao wa kuombea miito kusudi Mwili wa Kristo upate kujengwa.
Padri Ernest Mangwinda alizaliwa huko Namupa katika Wilaya ya Lindi Vijijini tarehe 10 Machi,1983 katika familia ya watoto nane, yeye akiwa mtoto wa wanne. Alianza masomo ya msingi hapo Namupa kabla ya kujiunga na Seminari Ndogo ya Namupa ambako alihitimu masomo ya Sekondari mwaka 1976.
Kwa kuwa bado alikuwa na nia ya kuwa padri, aliendelea na masomo ya Seminari Kuu Peramiho, Songea hadi Novemba 8, 1983 alipopadrishwa na Askofu Maurus Libaba(marehemu).
Kutokana na ugonjwa wa ngozi ambao ulimlazimisha kuhudhuria Kliniki huko Nyangao, na KCMC Moshi, uongozi wa Jimbo ulimpangia aishi Procure Lindi ambako aliweza kuhudumia Parokia ya Mtakatifu Fransisko Lindi, mpaka mauti yalipomkuta Agosti 28, huko kwenye Hospitali ya Sokoine Lindi ambako alipelekwa ili atibiwe.
Kwa mujibu wa taarifa za kitabibu, kifo chake kinaitwa “Cerebral Vascular Accident”, yaani, ajali ya kupasuka mshipa mkubwa kwenye ubongo kutokana na shinikizo kubwa la moyo, ambalo halitibiki.
Mazishi hayo yamehudhuriwa pia na Abate wa Ndanda, Plasido Mtunguja OSB, Abate mstaafu Padri Dionis OSB, na Mapadre wapatao 56 kutoka majimbo la Lindi, Mtwara, Tunduru Masasi na kutoka Jimbo la Anglikana Masasi, pamoja na idadi kubwa ya Watawa na waamini walei kutoka majimbo hayo.
Sista Suzan
Aidha Agosti 28, 2018 Mkurugenzi Mkuu wa Hospitali ya Bugando alitangaza kifo cha Mkurugenzi wa fedha na mipango wa Bugando Sista Suzan Bartholomew ambaye alifariki usiku wa kuamkia Agosti 28.

Raha ya Milele uwape Ee Bwana, na Mwanga wa milele uwaangazie, wapumzike kwa amani, Amina.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU