Fanyeni maamuzi sahihi juu ya imani yenu-Ask. Mdoe

Na Jimmy mahundi, Mtwara
WAAAMINI wa Jimbo Katoliki Mtwara wametakiwa kufanya maamuzi sahihi katika masuala ya kiimani na kuacha kutangatanga pasipo kufanya uchambuzi wa kina.
Hayo yamesemwa hivi karibuni na Askofu wa Jimbo Katoliki Mtwara Mhashamu Titus Mdoe wakati wa Ibada ya Misa Takatifu iliyoenda sambamba na utoaji wa Sakramenti ya Kipaimara katika Kanisa la Mtakatifu Paulo Parokia ya Majengo.
Askofu Mdoe amesema hayo kufuatia uwepo wa waamini wengi wanaohangaika na kuchukua maamuzi katika mambo yanayohusu imani pasipo kufanya uchambuzi na kubaini ukweli. “Kabla ya kufanya maamuzi fanyeni uchambuzi na kubaini baya na zuri, kisha baya liache” amesema Askofu Mdoe.
Aidha amebainisha kuwa wapo watu wengi katika nyakati hizi wanaotangatanga katika imani na kuwataka kuachana na kuhangaika bali wawe na misimamo ya kweli katika imani yao hiyo.
Pia katika nafasi hiyo, amewakumbusha wazazi na walezi kuwafundisha watoto wao kuchagua na kufanya maamuzi sahihi kwa kuwa huo ni wajibu wao.
Amewataka watoto wote jimboni humo kuishi katika imani zao na mafundisho wanayopewa kuhusu imani wazingatie kikamilifu pasipo wasiwasi wowote kwa kuwa imani yao siyo ya kubahatisha.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU