Ask Amani afafanua uvaaji wa shela siku ya ndoa

Na Pascal Mwanache
IMEELEZWA kuwa uchumba siyo kipindi cha kuvamia haki za ndoa bali ni kipindi cha wachumba kufahamiana, kuheshimiana na kutunza nidhamu, na hivyo haina maana kwa msichana ambaye hakutunza usichana wake kuvaa shela siku ya ndoa.
Hayo yamesemwa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Arusha Mhashamu Isaac Amani katika homilia yake Dominika ya 5 ya Pasaka hapo Aprili 29, 2018 katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Theresia wa Mtoto Yesu Arusha, ambapo amewasihi vijana kujitunza vizuri na kuwataka wazazi na walezi kuwasaidia vijana wao katika makuzi yao.
“Shela ina maana ya ubikira. Wale ambao wametunza ubikira mpka siku ya ndoa wavae shela. Watakaoruhusu ubikira utoke kabla ya ndoa wasivae shela, haina maana. Wanaovaa shela ni wale mabikira ndiyo maana ya shela, siyo unavaa tukuone tu” ameeleza Askofu Amani.
Askofu Amani ameyasema hayo alipokuwa anawahimiza wazazi na walezi juu ya umuhimu wa Shirika la Kimisionari la Utoto Mtakatifu wa Yesu kwa watoto akisema kuwa shirika hilo linawasaidia watoto kukomaa kiimani na kuwa wamisionari katika fikra zao.
“Jitunze. Na kama hauna matunzo usivae shela, haina maana. Akikushawishi mchumba mwambie ninataka nitunze hadhi yangu mbele ya Mungu, dhamiri yangu na pia kwa wazazi wangu. Mapenzi ya uchumba siyo kuvamia haki za ndoa hapana. Ni kufahamiana, kuheshimiana na kutunza nidhamu. Na anayekwambia tuharibuharibu kwanza huyo huyo anakuambia kuharibu kwake siyo jambo la ajabu. Ni ujumbe huo. Wavulana mjitunze vizuri na wasichana na wazazi msimamie” amesema.
Ataja namna bora ya kusherehekea kipaimara
Aidha Askofu Amani amewaasa wazazi kuwajengea watoto wao mazingira yatakayowajenga kulingana na mahitaji yao hasa wanaposherehekea komunio ya kwanza na kipaimara ambapo wazazi wengi wamekuwa na kasumba ya kuwafanyia watoto wao sherehe katika kumbi na mara nyingine nyakati za usiku.
“Zawadi ya kumpa mtoto wa komunio ya kwanza ni Biblia siyo simu. Mtoto wa Komunio ya Kwanza apewe Biblia kwa sababu ameshapata misingi ya kuingia mafundisho ya kipaimara. Hakuna furaha ya mtoto zaidi ya kukaa na watoto wenzake. Siku ya kipaimara watoto wakae na askofu na kupiga picha na ‘cheers’. Siku ya mtoto iwe ni ya mtoto na watoto mwenzake wafahamiane, tunawatengenezea mazingira waendelee kuwa pamoja na kujenga umoja wa kanisa, ni nguvu yetu hiyo” ameasa.
Pia amesema kuwa mavazi ya kuvaa siku za kipaimara kwa waimarishwa ni shati jeupe pamoja na suruali na sketi nyeusi na siyo shela kwa kuwa shela huvaliwa siku ya harusi tena huvaliwa na mwanamke aliye bikira.

Aelezea kaulimbiu yake
Akiielezea kaulimbiu ya utume wake “Mwondoko kuwajibika na kushirikiana katika Kristo” Askofu Mkuu Amani amewataka waamini jimboni humo kushirikiana na kujitathmini kiimani wako wapi, katika familia wako wapi, wanakwenda wapi na nini wafanye  ili kufikia malengo yao.
Amewataka wajifunze ushirikiano kama wa mchwa ambao hushirikiana kujenga kichuguu na kila mchwa hutengeneza tope akitumia mate yake na udongo ikiwa ndiyo mchango wa kila mmoja katika kichuguu.
“Tembo hathubutu kubomoa kichuguu anakiheshimu, ni kitu imara, kimejengwa kwa kuwajibika na ushirikiano. Kama mchwa ameweza kufanya hayo kwa nini sisi wenye zaidi ya mate na udongo tushindwe? Sisi tunaweza zaidi. Leo nazindua kaulimbiu hii ya awamu ya nne” amebainisha.


Comments

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU