Kazi ya mama ni kulea miito –Ask. Banzi

Na Dominic Maro, Tanga
Askofu wa Jimbo Katoliki Tanga Mhashamu Anthony Banzi amewapongeza wanachama wa Chama cha Mama wa Shauri Jema kwa kusaidia kulea na kukuza miito katika Kanisa.

Askofu Banzi amewapongeza akina mama hao hivi karibuni katika adhimisho la Ibada ya Misa Takatifu katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Anthoni wa Padua Chumbageni jimboni humo  walipokuwa wakisherekea jubilei ya miaka 25 ya umoja wao.
 Wanashirika hao ambao wameungana kutoka Jimbo Katoliki Tanga na Morogoro wameaswa kuendeleza malezi  kwa vijana kwa manufaa ya Kanisa la Mungu na nafsi zao.
“Msitishwe na changamoto mbalimbali zinazojitokeza. Bikira Maria ambaye ni msimamisi wa umoja wenu awasaidie katika hali zote kwa kufikia maisha ya utakatifu baada ya kufanya kazi kubwa hapa dunia ya kuwasaidia na kuonesha njia ya imani yenye ukamilifu mkuu,” amesema Askofu Banzi.
Pia amewataka wanawake wengine ambao hawajajiunga na umoja huo kujitokeza kwani  ni umoja wenye faida kwa manufaa ya Kanisa kwani kazi ya mama ni kulea.
Amewakumbusha wanaume kujiunga na wanawake hao kulea miito na pia kujiunga na  mashirika na Vyama vya Kitume ili wapate nafasi ya kujiombea na kuliombea Kanisa na dunia nzima.
Ikumbukwe kuwa misa hiyo ilitanguliwa na Mkutano Mkuu wa siku tatu wa kujadili na kupanga mikakati ya kusherekea jubilei ya mika 25 ya chama cha Mama wa Shauri Jema na wakihitimisha kwa Ibada ya Misa Takatifu.
Kwa upande wake Mwenyekiti wa chama hicho Mama Teodora Mtejeta ameeleza mafanikio wanayojivunia tangu umoja huo ulipoanzishwa miaka 25 iliyopita na Askofu Thelesphor Mkude wa Jimbo Katoliki Morogoro ikiwa ni kuendelea kufanya kazi ya kulea miito mbalimbali na kuongezeka kwa wanachama wapya.
“Sisi kazi yetu kubwa ni kujitoa katika Kanisa hasa kusaidia kulea miito na hili ndilo lengo la kuanzishwa kwa chama cha Mama wa Shauri Jema na hivi sasa tumeweza kuunganisha matawi mawili Tawi la Morogoro na Tawi la Tanga,” amesema Teodora Mtejeta.
Naye Katibu wa Mama wa Shauri Jema Jimbo Katoliki Morogoro Celina Komba amesema kuwa, umoja wao umelenga kuongeza wanachama wengi wapya mpaka wafikie 80 ifikapo mwaka 2019 kwani kwa sasa wapo zaidi ya 60.
Akina mama kutoka majimbo hayo wanaaswa kujiunga na chama hicho ili kulea miito katika Kanisa kwani mama ni mlezi katika jamii.


Comments

  1. Roho Mtakatifu awaongoze mzidi kufanya kazi kwa ushirikiano na kuenea sehemu nyingi katika Tanzania.

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU