Kila muumini awe mmisionari-Padri asisitiza

Na Ivetha Kimburu ± Dar es salaam

WANAUTUME wa Fatima hapa nchini, wameelezwa kuwa kupitia ujumbe wa Fatima uliotolewa na Bikira Maria kule Ureno alipowatokea Watoto wa Tatu, Russia, Fransisko na Yasinta wanaalikwa kuwa wamisionari wa kweli na hasa kuwaombea wale wote wasiomwamini Kristo, ili wapate kumwamini na kufuata matendo yake.
Wito huo kwa Wanautum hao wa Fatima umetolewa na Padri Evans Msechu, wakati akiadhimisha sadaka ya Misa Takatifu kwenye adhimisho la siku ya Bikira Maria Mama yetu wa Fatima iliyofanyika katika Parokia ya Msimbazi Jimbo Kuu Katoliki la Dar es salaam.
Padri Msechu ambaye ni katibu wa Ndugu wadogo wa Fransiskani amesema kuwa, Mama Bikira Maria ni mmisionari wa kwanza, na kwa kuwa Wanautume wa Fatima wanamwakilisha yeye hawana budi kuwa wamisionari katika maisha yao yote na mahali popote pale wanapokuwa.
Aidha ameongeza kuwa wanautume wa Fatima wanapaswa kutambua kuwa wao ni mabalozi, na kazi kubwa ya Balozi ni kuwakilisha jamii kubwa iliyoyuma yake, na sasa watambue kuwa wanayo kazi kubwa ya kuhakikisha wanaombea amani ndani ya familia, jumuiya parokia, taifa na hata ulimwengu mzima, na si kujiombea wao wenyewe tu.
Padri Msechu ameeleza kuwa, kwa kuwa wanautume wa Fatima ni mabalozi wa Mama Bikira Maria, wahakikishe watu wanamuona Bikira Maria pamoja na Yesu Kristo ndani ya mioyo yao kupitia kazi yao wanayofanya, matendo yao, na hata kuongea kwao.
“Wewe ndiwe balozi wa Mama  Maria, maana yake pale unapofanya kazi unamwakilisha Mama Maria, sehemu ambayo Maria alikuwa aende akafanye kazi wewe unafanya badala yake, kwa hiyo ongea yako iwe ni ya Kibira Maria, kazi yako unayofanya mtu atambue na amuone Kristo na Bikira maria ndani yako,” alisema Padri Msechu.
Padri Msechu amehitimisha mahubiri yake kwa kuwataka wanautume hao wa Fatima kuendelea kumuomba Mama Bikira Maria aendelee kuwasindikiza na kuwaombea,ili wahusianishe maisha yao na kile walichonacho na kufanya mageuzi ya ndani ya mioyo yao na si mageuzi ya nje, na pia waendelee kujikita katika kusali kwani dunia ya leo isipokuwa na amani watambue kuwa wao utume wa Fatima ndio shida kwamaana wameshindwa kusali zaidi.
Adhimisho la Misa takatifu siku ya Bikira Maria Mama yetu wa Fatima, lilitanguliwa na maandamano ya Rozari Takatifu, maungamo, mafundisho, pamoja na kuabudu na Ekaristi Takatifu, ambapo Padri Msechu alikuwa akishirikiana na Padre Gidion Peter Mboya Paroko Msaidizi wa Parokia ya Msimbazi ya Bikira Maria Mama wa Fatima.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU