Utabiri Wa Baba Mtakatifu Paulo Vi Watimia




Imekuwa ni kawaida sana kwa Mababa Watakatifu wakaliapo kiti cha Petro kutoa mafundisho kwa njia ya nyaraka, ziitwazo‘insiklika’ na kusambazwa kwa Maaskofu wote na makanisa yote dunia nzima pamoja na vyombo vya habari. Insiklika ni waraka unaosheheni mafundisho ya msingi ya kanisa. Mafundisho haya ni ya imani yanayogusa matatizo ya kijamii na kutoa msimamo wa kanisa mintarafu jambo fulani katika wakati fulani. Mfano wa insiklika hizi ni kama insiklika ya‘Evangelium Vitae’(Injili ya Uhai);‘Humanae Vitae’ (Juu ya Uhai), ‘Dignitatis Humanae’ Juu ya Utu wa Mwanadamu, ‘Populorum Progressio’ Juu ya Maendeleo ya Watu, ‘Evangelii Gaudium’ Juu ya Injili ya Furaha na nyingine nyingi.
Mwaka 1968, Baba mtakatifu Paulo VI aliandika insiklika iitwayo ‘Humanae Vitae'  ikijibu kiu ya watu ndani ya kanisa, mintarafu matumizi ya vidhibiti mimba, kama ni vyema ama si vyema kutumia vidhibiti mimba, na kuainisha njia bora za kupanga uzazi kwa njia ya maumbile kama Mungu alivyoratibisha.Hata hivyo ikumbukwe kuwa mnamo mwaka 1930, Umoja wa Makanisa ya Kianglikana katika mkutano wao wa Lamberth, ingawa walikubali kuwa, njia bora ya kupanga uzazi ni ile itumiayo mwenendo wa maumbile, lakini waliruhusu matumizi ya vidhibiti mimba kwa wanandoa wenye matatizo ya pekee. Ruhusa hii ilifungua milango kwa matumizi ya vidhibiti mimba hata pasipo matatizo yoyote, na hatimaye ukawa ndio mtindo wa kupanga uzazi kwa watu wa ndoa.
 Kutokana na ruhusa hiyo ya Waanglikana na kutokana na kuongezeka kwa vitisho dhidi ya taasisi ya ndoa, Baba Mtakatifu Pius XI, mnamo Decemba 31, 1930 alitoa tamko la Kanisa Katoliki kuhusu matumizi ya vidhibiti mimba.
"Kwa sababu yoyote, hata kama ni kubwa kiasi gani, haitaruhusiwa matumizi ya njia ambazo kwa asili yake ni ovu dhidi ya maumbile na kuzifanya zikubalike kimaadili kama vile zingekuwa njema. Kwa vile tendo la ndoa limeelekezwa kimaumbile katika uzao wa watoto, wale wanaoliharibu kwa makusudi na kuliondolea uwezo wake wanatenda dhambi dhidi ya maumbile na wanajiletea aibu na uovu wa ndani. (Casti Cannubii, Na 54)"
Katika kujenga hoja kwa nini matumizi ya vidhibiti mimba, vitisho dhidi ya taasisi ya ndoa, na vitisho dhidi ya ongezeko la idadi ya watu havikubaliki kiimani na kijamii Baba Mt Paulo VI alisema:
Kwanza; matumizi ya vidhibiti mimba yatafungua milango kwa watu kukosa uaminifu kwa kiapo cha ndoa  na pia wale walio nje ya ndoa kukosa uaminifu katika maisha yao. Wakati mwingine wanandoa wanatumia vidhibiti mimba bila kuwa na sababu. Mfano waweza kuta katika ndoa mume amesafiri kikazi hata miezi miwili lakini huku nyuma mke anatumia vidhibiti mimba hii ni kutokana na dhana kwamba haogopi uasherati wala magonjwa ya zinaa bali anaogopa mimba. Tunayoyashuhudia sasa hivi kama kuongezeka kwa matumizi ya vidhibiti mimba kama vitanzi, sindano na kusheheni kwa kondomu za aina mbalimbali kwenye maduka ya dawa kunadhihirisha kuwa kukosa uaminifu katika ndoa na wale wasio kwenye ndoa umekuwa mkubwa. Pia mambo kama kutoka nje ya ndoa yaani uasherati kwa lugha ya kisasa 'mchepuko' nao umeongezeka sana na kupelekea kuvunjika kwa ndoa hali ambayo huletwa na ubaridi wa vidhibiti mimba na chuki kwa tendo la ndoa kwa mume.
Matumizi ya vidhibiti mimba humjengea mtumiaji uhuru na mtumiaji kujisemea mwenyewe kuwa, mume au mke wangu hatajua, sitaweza kupata au kumpa mimba. Nitaendelea na masomo yangu kama kawaida. Nitaweza  kubadilisha wanaume au wanawake nipendavyo.
Pili; matumizi ya vidhibiti mimba yatasababisha mmomonyoko wa maadili kutokana na udhaifu wa kibinadamu, na hasa miongoni mwa vijana ambao wanakuwa katika hatari kubwa ya vishawishi vya ngono katika umri wao. Vijana wamekuwa wahanga wakubwa katika mmomonyoko wa maadili, huko mashuleni vijana na wanafunzi wetu pamekuwa sio mahali salama tena kwani wamekuwa wakifundishwa elimu ya ngono katika umri wao mdogo ambapo matumizi ya vidhibiti mimba yanahimizwa, elimu ya ushoga, kama katika kipindi cha mwezi mmoja uliopita katika taarifa iliyotolewa na Waziri wa Katiba na Sheria Mheshimiwa Dk Harrison Mwakyembe namna baadhi ya mashirika ya kigeni kwa kushirikiana na watu matajiri hapa nchini wanavyofanya vikao vyao usiku katika utekelezaji wa kuwafundisha wanafunzi mambo ya ushoga huko mashuleni. Jambo hili linatuogofya wazazi na walezi kwamba watoto wetu hawako salama tena.
Uzinzi na biashara ya ngono inaongezeka kila kukicha. Tunashuhudia katika jamii na sehemu tunamoishi jinsi vijana na watoto wetu walivyoharibika kwa kujikita katika mambo ya umalaya na uzinzi. Kumomonyoka huku kwa maadili kwa vijana kumesababisha kijana kukosa tunu ya usafi wa moyo pamoja na tunu nyingine kama kujikatalia, kujishinda na kujiheshimu.
Tatu; watu wanapozama katika mazoea ya vitendo vya kuepa mimba kwa matumizi ya vidhibiti mimba, hatimaye wanapoteza heshima kwa mwanamke, na hivyo kushindwa kumjali katika mahitaji yake ya kimwili na kisaikolojia, wanaweza kufikia mahali pa kumwona mwanamke kama chombo cha starehe, yaani cha kujifurahisha kibinafsi na tena si mwanamke  anayepaswa kuheshimika na mwenzi wa maisha. Mwanamke anafanywa kuwa chombo cha biashara za ngono, mfano tovuti mbalimbali zinatangaza biashara hii ya ngono, pamoja na mashirika mbalimbali ya biashara ya ngono yameanzishwa mfano nchini Ujerumani kwa sababu kuna anayeuza na anayenunua. Kwa sababu ya matumizi ya vidhibiti mimba inamfanya mwanamke wakati wote kuwa tayari katika kufanya tendo la ndoa, kwa kuwa hana hofu ya kupata mimba kitu kinachopelekea thamani yake kupotea.
Nne; ifahamike kuwa silaha hatari zinawekwa mikononi mwa watawala ambao hawajali mahitaji ya kimaadili. Kwa hiyo viongozi wa serikali watanyang’anya mamlaka wanandoa katika kupanga uzazi, badala yake serikali itawalazimisha watu kupanga uzazi kwa kutumia njia zile zisizokubalika kimaadili yaani kutumia vidonge vya majira, sindano za depo-provera, vitanzi, vipandikizi na kondomu.
Utabiri huu wa Baba Mtakatifu Paulo VI aliutoa katika insiklika, JUU YA UHAI au 'Humanae Vitae' iliyotolewa tarehe 25 Julai 1968 hatimaye umekamilika. Hii inatokana na mkutano wa kimataifa juu ya uzazi wa  mpango uliofanyika kwa wiki moja hapa Tanzania kuanzia Oktoba 31 na kumalizika Novemba 4, 2016. Mkutano huu uliandaliwa na shirika lisilo la kiserikali la FP 2020 kwa kushirikiana na GFF, ni ufuatiliaji wa utekelezwaji wa maazimio ya mkutano uliofanyika katika jiji la London mwaka 2012 uliofadhiliwa na Bill and Melinda Gates Foundation; likiwa na lengo ifikapo mwaka 2020 wanawake milioni 120 kutoka nchi za Afrika na Kusini Mashariki Asia ambao hawajapata huduma ya uzazi wa mpango wawe wamepata.
Katika ufunguzi wa mkutano huo wa FP2020 gazeti moja la hapa nchini la kila siku la tarehe 2 Novemba 2016 limemnukuu Waziri wa Afya alipokuwa anaufungua akisema, “Kiwango kikubwa cha mimba kati ya wasichana walio chini ya miaka 18 limekuwa tatizo kubwa ambalo tunahitaji kulishughulikia”. Kwa hiyo  matumizi ya vidhibiti mimba kwa Tanzania ili kufikia malengo ya kidunia ya uzazi wa mpango ifikapo 2021 sasa yataelekezwa  kwa vijana.
Baba Mtakatifu Paulo VI aliposema kuwa serikali itaingilia uhuru wa wanandoa katika kupanga uzazi; hili tunaliona sasa namna serikali inavyotumia nguvu nyingi katika kufanikisha hili, na tayari unabii umetimia. Serikali kwa kupitia Wizara ya afya imekuwa mstari wa mbele katika kuhamasisha watanzania watumie vidhibiti mimba yaani kondomu, vitanzi, vipandikizi na sindano za depo-provera chini ya mwavuli wa afya ya mama na mtoto na vijana. Hili limethibitika pale FP 2020 na Global Financial Facility walipoahidi kutoa fedha kiasi cha dola za kimarekani milioni 40 ili kuboresha vituo vya afya 100 vitakavyotoa huduma ya uzazi wa mpango.
Suluhisho la mimba za utotoni sio kuongeza matumizi ya vidhibiti mimba; la hasha! Matumizi ya vidhibiti mimba yanachangia ongezeko la vijana kujihusisha na umalaya na uhuni jambo linalochangia kuongezeka kwa mimba za utotoni. Suluhisho la kweli ni kuacha kuwafundisha watoto wetu na wanafunzi wetu elimu ya ngono.
Ndugu zangu Watanzania wote bila kujali dini, itikadi zetu tuje pamoja kuangalia ni namna gani tutasimama kidete juu ya matumizi ya vidhibiti mimba kwa watoto na vijana wetu.
Matumizi ya vidhibiti mimba kwa Tanzania ili kufikia malengo ya kidunia ya uzazi wa mpango ifikapo 2020 sasa yataelekezwa  kwa vijana.
Ni lazima tufanye jitihada ili kuwaepusha watoto wetu na madhara yatokanayo na hivi vidhibiti mimba.
Jambo la kuihimiza serikali yetu kupitia Wizara ya Elimu ni kuwa hapa tulipofika tunahitaji somo la maadili litakalofundishwa kuanzia shule ya msingi mpaka vyuo vikuu, ili tuwafundishe watoto wetu maadili mema na siyo umalaya kupitia vidhibiti mimba.
Kauli kuwa tuelekeze matumizi ya vidhibiti mimba kwa vijana ni kuhalalisha uzinzi na umalaya kwa watoto na wanafunzi wetu. Ni kusema fanyeni tuu uzinzi na umalaya lakini angalieni msipate mimba.

Erasto Kimonge
Mkufunzi,
Pro-life Tanzania.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU