‘Hifadhini vizuri nyaraka za kanisa’

ASKOFU wa Jimbo Katoliki Musoma Mhashamu Michael Msonganzila amewakumbusha maparoko wa Jimbo hilo kuhakikisha wanatunza kumbukumbu muhimu na nyaraka zote za kanisa, ili kuondoa migogoro ambayo imekuwa ikijitokeza baina ya walei na wahudumu  wa Kanisa. 

Ameyasema hayo wakati wa Misa Takatifu ya uzinduzi wa Parokia mpya ya Huruma ya Mungu Kigera, iliyofanyika Kanisani hapo, sambamba na kutabaruku Altare, kubariki waamini, kanisa na vitu vyote vilivyomo ndani na nje ya kanisa hilo.

Askofu Msonganzila amesema kuwa makanisa mengi yamekuwa yakiingia migogoro na wananchi (walei) kutokana na kutokuwepo kwa nyaraka muhimu za kanisa kutokana na maparoko ambao ndio wasimamizi wa eneo husika, kutotunza nyaraka hizo vizuri, kwa ajili ya kukumbukumbu za baadaye.

Amezitaja nyaraka muhimu ambazo maparoko wanapaswa kuhakikisha zinatunzwa vizuri kuwa ni pamoja na  kitabu cha wabatizwa wote pamoja na wasimamizi wao, kitabu cha waliopata kipaimara pamoja na waliopata kumunyo ya kwanza, kitabu chenye taarifa zote za waliofunga ndoa na kuwapatia vyeti vyao kwa kuwa vyeti ni mali ya Serikali,v itabu vya mahesabu ya Parokia (yaani mapato na matumizi)  kwa kufuata sheria zote za Serikali kuhusu wahudumu wa taasisi wanaolipwa mishahara pamoja na kutoa risiti.

Pia kitabu kinachoonyesha mali ya kanisa inayohamishika na isiyohamishika, kuweka alama za mipaka ya eneo lote la kanisa, kwani baadhi ya walei wana tabia ya kuingia katika eneo la kanisa mara wanaposikia kuwa kanisa limekuwa parokia ili kuibua migogoro, sambamba na kupiga picha za kumbukumbu wakati mabwana ardhi wanaweka alama za mipaka ya kanisa haraka.


Hata hivyo amewapa angalizo maparoko hao kuwa wakristo wengi hasa wakatoliki wamekuwa mbele sana katika mizozo mikubwa ya masuala ya ardhi katika maeneo ya kanisa hivyo hawana budi kuwaeleza ukweli wa mambo waamini wao bila kuwaficha japokuwa wapo watakaopenda kuambiwa ukweli na ambao hawatapenda kuambiwa ukweli, ila cha msingi wahakikishe wanayafanya hayo.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU