‘Teknolojia ya habari iwe fursa ya uinjilishaji’

IMEELEZWA kuwa kukua kwa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (ICT) kunapaswa kuwa chachu ya kupanuka kwa shughuli za uinjilishaji kupitia mitandao ya kijamii.
Hayo yameelezwa hivi karibuni katika mafunzo ya kuwajengea  uwezo wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano,  kwa wana mawasiliano kutoka nchi wanachama wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika Mashariki (AMECEA), yaliyofanyika katika ukumbi wa mikutano wa White House, Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Kurasini Jijini Dar es salaam.
Akifungua rasmi mafunzo hayo, Mwenyekiti wa Kamati ya Mawasiliano katika Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, Askofu Bernadin Mfumbusa, ameeleza kuwa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano imerahisisha upatikanaji na kubadilishana taarifa huku mitandao ya kijamii ikigeuka kuwa sehemu ya maisha ya mwanadamu.
Aidha Askofu Mfumbusa, ambaye pia ni Askofu wa Jimbo Katoliki Kondoa, amekumbusha juu ya umuhimu wa kutumia vyombo vya habari hasa mitandao ya kijamii katika kuinjilisha, kujenga madaraja na kuimarisha jamii katika nyanja mbalimbali.
“Ujumbe wa Papa Fransisko katika Siku ya 50 ya Upashanaji Habari Duniani, ambao ulikuwa na dhima ya ‘mawasiliano na huruma; makutano yenye tija’, unatualika sote kutathmini uhusiano uliopo baina ya mawasiliano na huruma. Papa anasema kuwa mawasiliano yana nguvu ya kujenga madaraja, kuwezesha watu kukutana na kushirikishana, na hivyo kuimarisha jamii” ameeleza.
Kwa upande wake Padri Gallus Marandu, aliyemwakilisha Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, ameeleza kuwa kukua kwa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano kunapaswa kusaidia jitihada za kushirikishana maadili ya Injili kwa ajili ya kuendeleza dhamira ya Kanisa katika uinjilishaji.

Mafunzo hayo yamehudhuriwa na wana mawasiliano kutoka Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Tanzania, Kenya, Uganda, Malawi, Ethiopia, na Zambia.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU