Huwezi kutenganisha utume wa walei na maendeleo ya Kanisa- Kard.Pengo asema

IMEELEZWA kuwa waamini walei nchini wamekuwa chachu ya maendeleo ya Kanisa kwa ushiriki wao kikamilifu katika mipango na utekelezaji wake katika hatua mbalimbali.
Hayo yameelezwa na Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo wakati akizungumza na waandishi wa habari kuelekea maadhimisho ya jubilei ya miaka 50 ya utume wa walei Tanzania, yanayotarajiwa kufanyika katika viwanja vya Msimbazi Center jijini Dar es salaam na kufikia kilele chake Juni 16, 2019.
Kardinali Pengo ameeleza kuwa walei hawapaswi kujiona kuwa ni watu wa kuambiwa tu kana kwamba hawana mchango wowote, bali wanapaswa kuona kuwa wao ni sehemu muhimu ya maendeleo ya Kanisa.
“Kabla ya Mtaguso Mkuu wa pili wa Vatikani waamini walei walisubiri watekelezewe kila kitu kana kwamba hawana chochote cha kutoa. Baada ya mtaguso huo Kanisa limetambua nafasi ya walei na hivyo ni lazima wajue kuwa wana sehemu muhimu ya kufanya, siyo tu kulipa zaka na kusikiliza maelekezo” ameeleza Kardinali Pengo.
Aidha Kardinali Pengo ametumia fursa hiyo kuwakaribisha waamini kutoka majimbo yote nchini kushiriki kikamilifu katika maadhimisho hayo kwa ajili ya kumshukuru Mungu kwa jubilei hiyo.
Pia ametoa mwito kwa waamini kushiriki matukio mbalimbali yanayotangulia kilele cha jubilei hiyo ikiwa ni pamoja na semina mbalimbali zitakazotolewa na maaskofu na watu walioandaliwa, ikiwa ni njia moja wapo ya kuadhimisha miaka 50 ya utume wa walei.
Kwa upande wake Katibu Mtendaji wa Idara yaUtume wa Walei ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) Padri Raphael Madinda ameeleza kuwa uwepo wa walei katika Kanisa umekuwa chachu ya kuongezeka kwa miito mitakatifu ambayo inachipuka kupitia familia.
Amesema kuwa kupitia familia ambao ndio walei ndiko Kanisa linapata miito mbalimbali kama vile upadri na utawa, huku akitoa wito kwa waamini walei kuendelea kuziimarisha familia zao kwani mchango wake katika ustawi wa Kanisa ni mkubwa.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU