Ask. Nyaisonga aongoza waamini Iringa kwenye Jubilei za Mapadri

askofu Mkuu wa Jimbo Kuu  Katoliki Mbeya Mhashamu Gervas Nyaisonga  hivi karibuni ameongoza waamini wa Jimbo Katoliki  Iringa katika maadhimisho ya jubilei mbalimbali za mapadri wa jimbo hilo.
Walioadhimisha Jubilei ni pamoja na Monsinyori Julian Kangalawe Pelate ambaye ameadhimisha miaka 50 ya Upadri.
Pia walikuwemo mapadri walioadhimisha Jubilei ya miaka 25 ya upadri akiwemo Padri  Richard Chatila Paroko wa Parokia ya Kihesa,  Padri Paul Msombe Paroko wa Parokia ya Ipogolo,  Padri Baptist  Duma Paroko wa  Parokia ya Mdabulo,  Padri Christopher Nyoni mhadhiri kutoka Chuo Kikuu cha Kikatoliki RUCU na Padri Cephas Mgimwa ambaye pia anafanya kazi Chuo Kikuu  cha Kikatoliki RUCU ambaye hakushiriki Misa hiyo yupo nje ya nchi kwa majukumu mengine.
Akitoa homilia katika Misa hiyo ambayo imefanyika katika ukumbi wa Seminari ya malezi Mafinga na kuhudhuriwa na Askofu wa Jimbo Katoliki Iringa Mhashamu Tarcisius Ngalalekumtwa, Askofu wa Jimbo Katoliki Ifakara Mhashamu Salitarius Libena na mapadri kutoka ndani na nje ya Jimbo pamoja na waamini, Askofu Nyaisonga amewataka wanajubilei hao kutambua kwamba bado hawajamaliza kazi hivyo  wanapaswa kuweka juhudi zaidi katika kutakatifuza ulimwengu.
“Ninawasihi mmbaki kuwa mashahidi  wa Injili katika ulimwengu. Tunawategemea kufundisha ukweli wa Injili na muwe mashahidi wa Imani yenu kama walivyokuwa Mashahidi wa Uganda,” amesema Askofu Mkuu Nyaisonga.
Maadhimisho hayo ambayo yameadhimishwa siku ya Sikukuu ya Mashahidi wa Uganda Askofu  Nyaisonga amesema kuwa matukio yote ya mashahidi hao hayatokani na kifo cha ushahidi bali maisha yao kwani waliishi kikamilifu na walikuwa tayari kumwaga damu kwa ajili ya imani yao.
“Sisi leo tunapomshukuru Mungu kwa hilo,  tunao mashahidi wengine ambao hawakumwaga damu,  bali wametoa jasho lao,  wamemtumikia Mungu kwa miaka 25 na 50 miaka hiyo si mchezo” amesema Askofu Nyaisonga na kuongeza;
“Mapadri hawa wanamshukuru  Mungu kwa kuwa hawana mastahili yoyote,  sisi leo tunawasifu kwasababu bila shaka miaka hiyo wamedhihakiwa kwa useja wao, ufukara, utii, maudhi, mambo mengi tu,  wameamini kwa dhati hata Mwenyezi Mungu amewatambua, wamevumilia na kuamini ndiyo maana tunawasifu na kuwapongeza leo.”
Amewalezea wanajubilei hao kuwa miaka hiyo 25 na 50 umri wao unawaambia wana imani na hadi sasa wanapenda wito wao na wameushikilia.
  Hamjamaliza kazi, mzidi kuita Roho ya Bwana iwaongoze. Mna wajibu wa kuendelea kuwa mashahidi wa sasa,” amesema.
Vile Vile amewataka waseminari ambao wanalelewa katika seminari hiyo nao pia wawe mashahidi kama msimamizi wao wa Seminari Mt Kizito na sio kumudu taaluma tu.
Akitoa neno la shukrani kwa niaba ya wanajubilei wenzake,  Paroko wa Parokia ya  Ipogolo Padri Paulo Msombe amesema wanamshukuru Mungu, wazazi jamaa na marafiki kwa malezi yao katika kuchochea wito wao.

“ Tunashukuru pia Askofu wetu Ngalalekumtwa kwa malezi yake tangu alipokuwa Rector  wa Seminari hii ya Mafinga hata sasa Askofu kwa malezi yake  ambayo yametusaidia kufika hapa tulipo,” amesema  Padri Msombe.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU