Askofu Nzigilwa apongeza Utume wa Halmashauri ya Walei Tanzania


Askofu Msaidizi wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam, Mhasham Euzebius Nzigilwa ameungana na waamini na viongozi wa Halimashauri ya Walei Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam katika kuadhimisha jubilei ya dhahabu ya miaka 50 ya utume wao.
Akitoa homilia yake wakati wa Ibada ya Misa Takatifu ya adhimisho hilo lililofanyika kwenye viwanja vya Msimbazi centre Dar es salaam, Askofu Nzigilwa amesema kuongezeka kwa imani nchini kumechangiwa kwa kiasi kikubwa na uwepo wa utume wa halimashauri ya walei.
 “Nia ya Askofu Mkuu wa Jimbo hili Mwadhama Polycarp Kadinali Pengo ya kutaka kujengwe nyumba za mapadri kwaajili ya kuwasogezea waamini huduma za kiroho kutoka kwa mapadri ilichagizwa kwa kiasi kikubwa na uwepo wa halimashauri ya walei.
Na utume wao tangu mwanzo umelipa jimbo letu nguvu ya kuinjilisha na kukua kwa imani,” amesema Askofu Nzigilwa.
Aidha ametoa wito kwa Halmashauri ya Walei Jimbo na kwa waamini wote waliobatizwa kuendelea kuishi kitakatifu katika wito wowote wanaoitiwa na Mwenyezi Mungu na wanao wajibu wa kuulinda.
Amesema ipo miito mingi na miongoni mwake ni wito wa kuwa watakatifu ambao amepewa kila Mkristo mbatizwa sanjari na wito wa uinjilishaji unaomgusa kila mbatizwa na kama Yesu alivyoagiza na kufundisha aliposema muwe watakatifu kama Baba yenu wa mbinguni alivyo mtakaifu,enendeni ulimwenguni kote mkaihubiri Injili na aliposema kama Baba alivyonituma mimi,nami nawatuma ninyi, ni wazi kuwa kwa mafundisho hayo ya Yesu kila mtu anatumwa wito wa uinjilishaji.
“Ndugu zangu  utakatifu wa maisha ndiyo silaha na nyenzo ya uinjilishaji na maisha hayo hayo matakatifu yanafundisha zaidi kuliko mambo tunayofundisha na kufundishwa.
Sasa ni wakati wa kila mbatizwa kujitahidi kujitakatifuza na kuyatakatifuza malimwengu,”amesema.
Ameongeza kuwa katika kujitakatifuza na kuyatakatifuza malimwengu ni sharti kila mmoja apambane ipasavyo na vikwazo vitakavyomfanya asitekeleze hayo na kushindwa kuishi kitakatifu.
Amevitaja miongoni mwa vikwazo huku chakwanza kikiwa ni watu kusikiliza na kutekeleza maelekezo ya ibilisi jambo ambalo ni kovu kubwa linalopelekea kushindwa kujitakatifuza na kuyatakatifuza malimwengu kwa kuishi kitakatifu.
Pia Askofu Nzigilwa amewaasa waamini na watu wote kuacha tabia ya kuyapelekea maelekeo yao kwa wengine badala yake kila mtu anapofanya kosa akiri kosa lake na si kutafuta kisingizio kwa wengine kama walivyofanya Adamu na Eva kwenye bustani ya edeni walipokula tunda ambalo hawakutakiwa kula na kila mmoja ajue anapofanya hivyo anasikiliza na kutekeleza maagizo ya ibilisi.
“Wanadamu huona haraka makosa ya wengine kuliko mapungufu yao wanasahau fundisho la Yesu ambalo anatufundisha kuona mapungufu na makosa yetu wenyewe na si ya wengine na bila kujua kwamba jambo hilo litawafanya kutokuishi kitakatifu,” amesema.
 Amesema bila kusimama imara  kazi ya uinjilishaji na kuuishi utakatifu itakuwa ngumu kwasababu ni lazima kila mmoja apambane na hila za ibilisi kwamaana utakatifu ni zawadi na ni miongoni mwa matunda ambayo Mungu ametupatia hivyo ni wajibu wa kila mtu kuupalilia utakatifu na ni kwanamna gani atastawisha mbegu hiyo maishani mwake.
Wakati huo huo Mwenyekiti wa harimashauri ya walei Jimbo Kuu Katoliki Dar es salam Ndg.Richard Sillo amemshukuru Askofu Nzigilwa kwa kuwakumbusha wajibu wao na wao wanaahidi kwamba wataendelea kuutumikia wajibu wao waliopewa kwa kushirikiana na wengine.
Jimbo Kuu Katoliki  Dar es salaam limeadhimisha jubilei ya dhahabu ya miaka 50 ya halimashauri ya walei kijimbo kabla ya kilele cha kitaifa kufanyika June 16, 2019 kwenye viwanja vya Msimbazi Centre Dar es salaam na kukusanya waamini wa majimbo yote 34.
Maadhimisho hayo yatakuwa ya kwanza tangu kuanzishwa kwa halimashauri ya waei mnamo tarehe 24 June 1969.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU