Benki ya Mkombozi yafungua tawi Iringa




Na Getrude Madebwe, Iringa
Benki ya Biashara ya Mkombozi imefungua tawi mkoani Iringa ikiwa ni utekelezaji wa mipango ya Benki hiyo kupanua huduma zake ili kuwahudumia wananchi kwa ukaribu.
Akifungua tawi hilo, Askofu wa wa Jimbo Katoliki Iringa Mhashamu Tarcisius Ngalalekumtwa amewataka waamini wa jimbo hilo, wananchi na watu wenye mapenzi mema kuitumia Benki ya biashara ya Mkombozi ambayo imeanza kutoa huduma zake mkoani humo.
Benki hiyo inatoa huduma mbalimbali za kibenki ikiwa ni pamoja na kutoa mikopo kwa vikundi, mtu binafsi, taasisi na mashirika mbalimbali.
Tawi hilo la Iringa ni kati ya matawi 10 ya Benki hiyo lengo ikiwa ni kuenea nchi nzima.
Awali, Askofu Ngalalekumtwa ameyabariki majengo ya Benki hiyo yaliyopo kwenye Chuo Kikuu cha Kanisa Katoliki cha Ruaha (RUCU) na amesisitiza umuhimu wa kuweka akiba kwenye benki.
“Tulitamani sana kuidhisha lile ambalo tumeidhinisha leo hii, benki ambayo tumeishughulikia sasa imefunguliwa hapa kwetu, ni nafasi ya benki hii kutulea huduma kwa karibu na sisi wananchi tujijengee utamaduni wa kuweka akiba  kwa matumizi mbalimbali,” amesema Askofu Ngalalekumtwa.
Aidha amewataka watendaji wa benki hiyo kuwa wabunifu na kutoa huduma kwa weledi kulingana na taratibu za benki.
Mkurugenzi Mtendaji wa Benki hiyo Bw. George Shumbusho amesema kwamba Benki hiyo mwaka huu Agasti 27 itakuwa ikiadhimisha miaka 10 tangu ianzishwe na Kanisa Katoliki Tanzania kutoa huduma kwenye maeneo mbalimbali nchini.
“Ndoto yetu ya kutoa huduma nyanda za juu kusini imekamilika ni wazi pia uchumi wa Iringa na watu wote wa  maeneo haya utazidi kuimarika baada ya kufungua benki hii hapa kwenu,” amesema Bw. Shumbusho .
Amesema kwamba kutokana na benki hiyo kuadhimisha miaka hiyo 10 ni  wazi kwamba benki hiyo ni komavu katika kutoa huduma kwa kiwango kinachoridhisha hivyo wamejipanga vizuri kutoa huduma bora zaidi.
Ametoa ombi kwa wakazi wa maeneo hayo kuitumia benki hiyo ambayo ina weledi mkubwa kwenye huduma za kibenki.
Makamu Mkuu wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki Ruaha RUCU, Dr Pd. Pius Mgeni amesema kwamba hakuna Benki ambayo ina jina kubwa kama Benki ya Mkombozi kwani imekuja kuwakomboa wananchi wa mkoa huo kiuchumi.
Pd. Mgeni amesema kwamba wapo tayari kushirikiana na benki hiyo katika kuimarisha uchumi wa Iringa.
Akizungumza na Gazeti hili, Meneja Masoko wa benki hiyo Bw. Andrew Chimanzi amesema kuwa, wamefungua milango ya benki hiyo kwa wateja wao ambao walikuwa wakisubiri kwa muda mrefu huduma za benki hiyo.
“Hii ni benki ya biashara ina kibali cha kufanya huduma zote za kibenki ikiwemo, kufungua akaunti, mikopo kwa wafanyakazi, mikopo mikubwa na midogo na kwa wajasiriamali wadogo pia.
Wito wangu kwa wana Iringa waje tuwahudumie, wafanyakazi wetu wana weledi wa kutoa huduma za kibenki hivyo tunawakaribisha,” amesema Bw. Cimanzi.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU