MAENDELEO HAYALETWI NA SIASA ZA UADUI- ASKOFU NKWANDE



Viongozi wa siasa nchini wameaswa kuchukulia changamoto walizonazo kuwaunganisha  kwa maslahi ya taifa badala ya kujenga uadui.

Mhashamu Askofu wa Jimbo katoliki Bunda Renatus  Nkwande amezungumza na gazeti hii juu ya mustakabali wa taifa baada ya mvutano wa UKUTA na wabunge wa vyama pinzani kukubali kuingia bungeni kwa heshima ya viongozi wa dini na Spika wa Bunge Job Ndungai

Askofu Nkwande amesema mustakabali wa taifa hili utakuwa hasi kama serikali itawaona wapinzani kitu cha bure. Kadhalika kama wapinzani watakuwa wanakosoa kila kitu serikali inachofanya tena kwa ushabiki wa maandamano. Amesema hayo ni mawazo dhaifu na haoni kama demokrasia inayotafutwa pamoja na maendeleo ya nchi hii yatapatikana kwa namna hiyo.

“Watawala wasifikiri kwa kuwadhoofisha wapinzani ndipo taifa litapata maendeleo na amani. Utawala mzuri unachukua changamoto kama sehemu ya kuimarika na kuwaacha wapinzani wafanye yao kwani kuitwa wapinzani lazima wakosoe utawala aidha kwa propaganda zao ama kwa maendeleo ya taifa.

Vilevile wapinzani wasifanye hoja zao kuwa sheria ambayo haipingwi na wasikosoe kila kitu. Wawe wavumilivu, wenye subira kwa ajili ya maendeleo ya taifa. Upinzani si kukataa kila kitu tu,” ameeleza Askofu Nkwande.

Amesema nchi ni ya kila mwananchi, na ni wajibu wa kila mwananchi kulinda amani na utulivu uliopo kwa manufaa ya sasa na ya baadaye.

Aidha baadhi ya viongozi wa dini wameeleza kuwa, ijapokuwa wabunge wapinzani wamekubali kuahirisha UKUTA na kuingia bungeni kwasababu ya kuwasubiri wakazungumze na rais inaonyesha kuwa wamekubali ushauri kwa masharti.
Iko hoja moja kuwa, endapo viongozi hao hawatafanikiwa kuonana na rais watarudia misimamo yao ya awali.
Kumbe kuwashawishi CHADEMA na serikali kufanya maridhiano ni kutimiza wajibu wao wa kuhakikisha amani ya nchi inadumu na kuondokana na dhana ya viongozi wa dini kutafuta usuluhishi badala ya kuacha nchi iingie katika machafuko.
“Baadhi ya watu wanachukulia suala la maandamano kama kitu kidogo lakini ingefaa wakajifunza kutoka katika mataifa mengine. Heri kuzuia moto kuliko kupambana na moto.

Sisi maaskofu, wachungaji na masheikh  ni washauri tu hivyo pale tunaposhauri na kukubaliwa ushauri wetu kwa masharti pia kuna ulakini.

Kuambiwa tunakubaliana kuahirisha maandamano kwa muda fulani ili mkazungumze na rais ni kama kushurutishwa kufanya interesti za vyama. Sisi ni viongozi wa dini tulio na dhamana ya kulinda maadili na imani za watu si siasa. Hivyo ningependa serikali pamoja na vyama vya siasa kutusikiliza kama washauri badala ya kutupa masharti,” ameeleza kiongozi mmoja wa dini ambaye hakupenda kutajwa jina lake.
Amesisitiza kuwa, viongozi wa dini pia wanapaswa kufahamu wajibu wao lakini si kuwa na interesti na chama flani ama upande mmoja wa mvutano. Wakiwa ni wanachama wa baadhi ya vyama hatutaweza kushauri vizuri na serikali haitapata ushauri unaofaa.
 Ameiasa serikali kuwa imara, kutoshindana na vitu vidogovidogo ambavyo vinapoteza muda badala ya kufanya kazi za maendeleo.

“Upinzani uachwe ufanye yake na serikali ifanye yake. Serikali ni kama inaweka makucha na kutumia nguvu nyingi kupambana na vitisho ambavyo kimsingi vilikuwepo tangu enzi za mwanzo wa mfumo wa vyama vingi.
Wapo viongozi wa siasa waliokuwa wakivuma sana kipindi kile lakini hata Nyerere mwenyewe aliwaacha wafanye yao na yeye akizidi kujiweka imara.” Ameeleza kiongozi huyo.
Amewaasa wapinzani kufanya kazi yao ya kuikosoa serikali kwa subira na uvumilivu bila kuhatarisha amani ya taifa.
Kuandaa polisi na jeshi kupambana na vitisho vya wapinzani ni  kuleta woga wa kivita kwa wananchi. Kadhalika kuandaa maandamano kwa kutumia nguvu na kauli za vitisho kunaleta pia woga wa kivita wa wananchi. Hivyo ninawasihi wanasiasa kufanya kazi zao kwa subira na uvumilivu.
Kubwa zaidi ni serikali kuangalia inapambana na nani. Kuna mambo ambayo wapinzani lazima wayafanye hivyo isiogope. Pengine wapinzani wameshajua kuwa serikali inaogopa changamoto ndio maana wanatishia ili kuifanya serikali dhaifu. Pia pengine serikali ina washauri wabovu ambao wanaweza kuidhoofisha serikali badala ya kuipa nguvu.

Ajenda yetu iwe moja tu, ‘kulijenga taifa.’ Si kitu kingine. Tutumie busara za mwalimu ili taifa liende mbele kimaendeleo. Wapinzani wasiogopwe wala wasichukuliwe kama maadui wa serikali. Serikali isionekane haifanyi chochote. Pale wanapofanya vyema wapewe motisha na wapinzani kusonga mbele badala ya kuidhoofisha serikali kwa kauli za vitisho na kupoteza muda kukimbizana barabarani na mahakamani.
Tufanye shughuli za maendeleo kama watanzania na kuacha itikadi za vyama pembeni,” Amesistiza Kiongozi huyo. Pia alivishauri vyombo vya dola kuongoza nchi kwa mujibu wa sheria na kanuni zinazosimamiwa na Katiba ya nchi bila kukandamiza demokrasia.
Amesisitiza kuwa, hayo lazima jamii hususani wanasiasa wayatafakari kwani bila hekima baada ya UKUTA na kususia vikao vya bunge linaweza likatokea jingine kubwa zaidi litakaloushtua ulimwengu.

 Na Sarah Pelaji, Dar es Salaam


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU