Katibu Mkuu TEC: Wananchi msikebehi maelekezo ya serikali dhidi ya corona


JAMII imetakiwa kutokuzikebehi na kuzibeza juhudi  zinazofanywa na serikali katika kukabiliana na maambukizi ya ugonjwa hatari wa covid-19 unaosababishwa na virusi vya corona, badala yake itekeleze kwa vitendo maagizo na miongozo inayotolewa.
Rai hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Padri Charles Kitima katika mahojiano maalum na vyombo vya Habari nchini, yaliyofanyika katikati ya juma ofisini kwake Kurasini jijini Dar es Salaam.
Amesema, Kanisa Katoliki nchini linaridhishwa na hatua zinazofanywa na serikali kupitia Wizara ya Afya katika mapambazo dhidi ya ugonjwa huu ulionea sehemu mbalimbali duniani, hivyo akasisitiza kwamba hakuna sababu ya baadhi ya watu ama makundi ya kijamii kuzibeza na kuzikebehi juhudi hizo.
Katika kusisitiza zaidi amesema “Tuiache Serikali ifanye kazi yake kwa kutumia wataalam wa afya iliyonao na kila mmoja kwa nafasi yake, atoe ushirikiano kama inavyotakiwa…hili siyo tatizo la kukebehi wala kufanyia mzaha kwani  linagusa afya za wananchi,”.
Ili kudhibiti zaidi kasi ya maambukizi, Padri Kitima amesisitiza kila mwananchi kujilinda mwenyewe na kuwa  mlinzi wa mwingine hasa kwa kukubali kuchukua hatua kama inavyoelekezwa na wataalam wa afya  mojawapo ikiwa ni matumizi ya vitakasa mikono na kuwahi hospitalini pale mtu anapohisi mabadiliko ya mwili hasa mafua yenye kuambatana na homa kali na dalili nyinginezo.
Hata hivyo licha ya kukiri kuwa Tanzania haiko vibaya sana kitakwimu katika kasi ya maambukizi  ya covid-19 hasa kutokana na hatua zilizochukuliwa, lakini ameishauri serikali kuendelea kusimamia na kuiboresha miongozo hiyo ili ilete matokeo chanya zaidi.
Kuhusiana na taarifa ya kimtandao iliyotolewa hivi karibuni kutoka Shirika la Afya Duniani (WHO) na kuripotiwa na Gazeti la Washington Post la nchini Marekani, kwamba katika kipindi cha wiki mbili zijazo yaani kuanzia April Mosi, 2020, kasi ya maambukizi ya ugonjwa huu barani  Afrika itaongezeka zaidi sababu kubwa zikitajwa kuwa ni ukaribu uliopo baini ya nchi za Afrika na China na ukosefu wa vipimo, lakini Padri Kitima akawatoa hofu Watanzania kkuwa wasitaharuki kwa kupata taarifa za kimtandao, badala yake zaidi wasikilize kile kinachosemwa na serikali yao.
“Serikali yetu ina wataalam wa afya hivyo Watanzania tusiwe na taharuki kusikiliza taarifa za kimtandao , badala yake tufuate mwongozo tunaopewa na serikali yetu yenyewe kwani anayetafasiri taarifa sahihi za kiafya toka vyanzo mbalimbali ni chombo hiki pekee,” amesisitiza.
Amesema, kwa sasa halisi ilivyo taarifa kutoka vyanzo mbalimbali zitatolewa lakini akasema zinatakiwa kuchujwa tena kiutaalam na katika kusimamia hili, hata serikali yenyewe tayari  imetoa maelekezo kuwa atakayetoa taarifa kuhusu corona ni Wizara ya Afya tu.
Katika kuhakikisha inatekeleza kwa vitendo agizo la serikali, anasema Kanisa Katoliki upande wake, tayari limechukua hatua madhubuti kudhibiti kasi ya ugonjwa huu kwa kuweka vitakasa mikono maeneo mbalimbali kuzunguka maenneo ya makanisa, kutokuweka maji ya baraka kwenye milango ya Kanisa, kubadilisha utaratibu wa kukomunika  pamoja na kuhakikisha benchi za kukalia kanisani zinasafishwa kwa kutumia dawa na sabuni maalum ya kuuwa wadudu, vitu ambavyo pia kanisa limekuwa likiwasisitiza waamini wake wakivitumia kwenye familia  zao.

Covid - 19 ni ugonjwa unayoisumbua dunia kwa sasa ambapo hadi kufikia Aprili Mosi, 2020 takribani watu 935,197 walikuwa wameambukizwa, kati yao 47,192 tayari walikuwa wamepoteza maisha. Katika idadi hiyo, waliyopona ni 193,989 ikilinganishwa na watu 994,016 wanaondelea kupatiwa matibabu kati yao 35,478 wakiwa mahututi.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU