Mamia wamzika Padri Mwechibindu




Na. Philipo Josephat - Dsm
Mamia ya waamini kutoka Parokia mbalimbali za Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, mapadri, watawa na maaskofu kutoka majimbo mbalimbali nchini na viongozi mbalimbali wa serikali  wamejitokeza kumzika marehemu Padri Andrew Mwachibindu aliyefariki katika Hospitali ya Taifa ya Muhimbili usiku wa January 12, 2019.
Akiongoza Ibada ya Misa Takatifu ya kumwombea marehemu kabla ya mazishi yake yaliyofanyika katika Kituo cha wafia dini Pugu Askofu Mkuu Mwandamizi wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam Mhashamu Yuda Thadei Ruwaichi amemtaja marehemu kama mtu aliyekuwa mtulivu, mwenye nidhamu na mipango chanya ya utumishi.
Aliyeongozwa na uchaji wa kimungu na mchungaji msikivu aliyependa kufanya yote vema.
Amesema katika maisha mwanadamu anapitia magumu na mateso mazito na anapokabiliwa na mateso hayo huwa anakuwa na hofu hivyo kila mwanadamu anapaswa aongozwe kwa imani yake kwa Kristo anapokabiliwa na kifo.
Ameongeza kuwa wakristo wote hawanabudi kuishi kama wana wa Mungu kwa kumuangaza Kristo katika maisha yao yote hapa duniani bila kusahau kukumbushana na kuhimizana kumwongokea Mungu.
“Ayubu alipata mateso na mahangaiko mengi sana kupitia hayo alipata ushauri mwingi kutoka kwa watu waliodhani pengine ushauri wao ungeweza kufanya aondokanae na mateso lakini  Ayubu alishikilia imani ya kumpenda Mungu katika mahangaiko yake yote” amesema.
Pia ameongeza kuwa kwa namna hiyo ya mateso aliyoyapitia Ayubu bila kuwa na mashaka na Mungu viyo hivyo na kila mwanadamu atambue kwamba uhai wa binadamu ni mali ya Mungu na kwa namna ya pekee amshukuru Mungu.
Askofu Ruwaichi amewatahadharisha watu ambao huwaondolea uhai wenzao wakisema wanawaonea huruma wasiteseke katika mateso yanayowakabili na kusema kwamba mtu wa Mungu ni lazima ateseke hivyo wanaofanya hivyo pengine hawamjui vizuri Kristo.
Kwa upande wake Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki  Dar es Salaam Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amesikitishwa na kifo cha Padri Andrew Mwechibindu akisema kwamba alipokea taarifa za kifo akiwa nchini India na alimwomba Mungu amsaidie aweze kufika siku ya mazishi na Mungu amemsaidia kufika katika mazishi hayo.
Ameongeza kuwa kwa nyakati tofauti alimpeleka marehemu katika Parokia ya Mafia akidhani angeweza kupumzika kulingana na hali ya upepo wa huko lakini ikawa tofauti kwake. Mwadhama pia ametoa pole kwa wazazi, ndugu, jamaa, mapadri na watawa wote wa jimbo hilo kwa msiba huo mzito.
Kwa upande wake kaka wa marehemu Ndugu John Simon Mwechibindu amemshukuru Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo, Maaskofu wote wa Jimbo Kuu Dar es salaam, mapadri na kwa namna ya pekee walivyofanya kazi ya utume pamoja na marehemu Padri Andrew Mwechibindu na kusema kwamba Kanisa limepata pigo kubwa sanjari na familia yao kwa sababu ni muda mfupi wamewapoteza dada zao wawili kwa hiyo kufariki kwa padri Mwechibindu ni pigo la pili.
Marehemu Padri Andrew Mwechibindu  ambaye alizaliwa January 02, mwaka 1965 akiwa ni mtoto wa tatu kati ya watoto nane wa familia ya mzee Mwachibindu alikuwa anasumbuliwa na maradhi ya moyo yaliyosababisha ashindwe kufanya kazi.
 Akiwa hai amehudumia parokia mbalimbali zikiwemo Mburahati, Magomeni, Mafia, Mikocheni, Mbezi Beach na mpaka mauti yanamkuta alikuwa katika parokia ya Mikocheni alipokuwa akisubiri kuhamia katika Parokia ya Mwanagati kama Paroko.
Mazishi hayo yalihudhuriwa na Raisi wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Mhashamu Gervas Nyaisonga wa Jimbo Kuu Teule Mbeya, Askofu Edward Mapunda wa Jimbo Katoliki  Singida, Askofu Titus Mdoe wa Jimbo Katoliki Mtwara, Askofu Yuda Thadei Rwaichi Mwadhama Polycarp Kadinari Pengo na Monsinyori Deogratias Mbiku .


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU