Moto wateketeza nyumba ya Mapadri Walezi wa Seminari Kuu ya Segerea



Na Sarah Pelaji, Dar es Salaam
Moto    umeteketeza  nyumba ya mapadri majalimu na walezi katika Seminari Kuu ya Mtakatifu Karoli Lwanga-Segerea iliyoko jijini Dar es Salaam majira ya saa nne na nusu usiku Januari 15 mwaka 2019.
Kwa mujibu wa Gombera wa Seminari  hiyo Padri Tobias Ndabhatinya chanzo cha moto ni tatizo la umeme lililosababishwa umeme kurudi kwa nguvu baada ya kukatika.
“Ni kawaida yetu kila jumatano jioni tunakutana ili kushirikishana masuala mbalimbali ya maisha yetu pamoja na kazi zetu. Wakati tunaendelea na  hilo ghafla tukasikia harufu ya kitu kinachoungua na baada ya sekunde chache tukasikia mlio kama kitu kilicholipuka. Kumbe ulikuwa ni moto ambao umeshaanza kuwaka kwenye ghorofa ya kwanza, ambapo kuna vyumba vyetu vya kulala. Ndipo tukasaidiana pamoja na wanafunzi kutoka nje na kusaidia wale waliokuwa vyumbani washuke. Kisha tukawasiliana na Jeshi la Zima Moto ambalo lilifanya kazi yake hadi kuzima moto huo,” ameeleza Gombera Tobias.
Amesema bado thamani ya mali zilizoungua hazijajulikana ingawa moto huo umeteketeza vyumba 14 vya mapadri hao na hakuna mali iliyookolewa katika vyumba hivyo.
Pia ameeleza kuwa, hakuna aliyejeruhiwa wala aliyefariki katika ajali hiyo. Amewashukuru  waseminari wa Seminari hiyo Kuu kwa ujasiri wao  na kutumia akili na nguvu kuwaokoa baadhi ya mapadri wao waliokuwa ghorofani hadi wakafanikiwa kuwatoa salama.
Pia waseminari hao walifanikiwa kuokoa magari ya seminari hiyo ambayo waliyasogeza bila kuyasha maana walikuwa hawana funguo hivyo waliyasukuma na mengine waliyabeba ili kuyaweka mahali salama yasije kuungua na kuteketea kwa moto.
Aidha amewashukuru majirani ambao waliwapa ushirikiano na wote waliofika kuwapa pole kwa ajali hiyo.
Hata hivyo baada ya taarifa  ya ajali hiyo kufika katika Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania, maaskofu  waliweza kutembelea seminari hiyo asubuhi ya Januari 16 mwaka huu ili kutoa pole kwa  mapadri hao wakiongozwa na gombera wa seminari hiyo, waseminari pamoja na wafanyakazi wengine.
Akitoa pole kwa niaba ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania TEC, Makamu Rais wa Baraza hilo (TEC) Mhashamu Flavian Kassala amewapa pole mapadri hao kwa  ajali hiyo iliyoteketeza mali zao na kuachwa  bila malazi na mavazi pamoja na mali nyingine walizokuwa nazo ambazo ni nyenzo za kufundishia.
“Kwa niaba ya TEC ninatoa pole nyingi kwenu mapadri na waseminari wote kwa ajali hii ingawa tunamshukuru Mungu tumewakuta salama maana hili ni tuko la kutisha.
Tumeona na tumeshuhudia jinsi moto ulivyoteketeza jengo hili lakini tunaomba muwe watulivu wakati masuala mengine yanaendela kufanyiwa kazi na maaskofu wenu ili mapadri wapate mahitaji msingi ya mwanadamu na mambo mengine yanayohitaji maamuzi ya haraka,” amesema Askofu Kassala.
Pia amewapongeza waseminari wa seminari hiyo kwa moyo wa kujituma hata wakaweza kuwaokoa mapadri kwa mbinu ambazo sinastaajabisha.

Pia kunusuru mali za seminari mfano magari kwani waseminari hao waliweza kuyasogeza kwa kuyabeba na mengine kuyasukuma maana walikuwa hawana funguo.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU