Maaskofu Katoliki Tanzania wapewa mafunzo juu ya Uongozi Bora




Na Sarah Pelaji, Dar es Salaam
Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC) kwa ushirikiano na Umoja wa Mabaraza ya Maaskofu Afrika Mashariki AMECEA na Missio, wametoa mafunzo kwa Maaskofu wa Kanisa Katoliki juu ya uongozi Bora.
Mafunzo hayo   ya siku tano yamefanyika kuanzia Januari  14-19, mwaka huu  katika Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Kurasini jijini  Dar es Salaam.
Maaskofu hao wanajengewa uwezo juu ya Uongozi na  Usimamizi wa taasisi, Uongozi Endelevu; Umoja wa Kanisa Katoliki pamoja na Ushauri na Usimamizi.
Awali Katibu Mkuu wa AMECEA Padri Anthony Makunde ameeleza kuwa, mafunzo hayo ni ya awamu ya pili  ambapo awamu ya kwanza yalikuwa yanafadhiliwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Marekani sasa awamu ya pili yanafadhiliwa na Baraza la Maaskofu Katoliki Ujerumani kupitia shirika lao la Missio.
Aidha ameeleza kuwa alifanya safari  na Rais wa AMECEA Mhashamu Charles Kasonde kwenda kukutana na Rais wa Missio Aachen, Makamu wake na Afisa  wa Ushirikiano wa Kimataifa ili kujitambulisha lakini pia kuendeleza awamu ya pili ya mafunzo kwa maaskofu na wasaidizi wa karibu wa maaskofu katika ukanda wa AMECEA pamoja na miradi mingine inayotekelezwa na AMECEA kwa kufadhiliwa na Missio.
“Ndiyo maana tupo hapa timu ya AMECEA tukishirikiana na TEC ili kufanikisha mafunzo haya ya siku tano,” ameeleza Padri Makunde.
Aidha ameeleza kuwa, amepewa wajibu wa kuwakumbusha maaskofu wote kuhusu mafanikio ya AMECEA tangu ilipoanzishwa miaka 58 iliyopita.
“Tunajivunia kwa kutembea pamoja hadi sasa tumefikisha miaka 58 tukiwa na ongezeko la waamini wabatizwa katika ukanda huu wa AMECEA.
AMECEA imezaa Chuo Kikuu cha Afrika Mashariki, Chuo cha AMECEA cha Kichungaji na Chuo cha Mwenyeheri  Bakanja.
Kumekuwa na ongezeko la jumuiya ndogondogo pamoja na mashirika ya kitawa kwa wanawake na wanaume,” amesisitiza.
Amewataka Maaskofu kutathmini maono ya waanzilishi wa AMECEA ambao walitaka kutembea pamoja kwa kuwa na mbinu na mikakati ya pamoja ya kichungaji.
Kumbe ilikuwa ni ari ya waasisi wa AMECEA kuwa na umoja na ushirikiano kwa ajili ya maendeleo ya ukanda wa AMECEA.
Pia kuna ongezeko la Maaskofu, majimbo na mapadri katika ukanda wa AMECEA.
Hivyo maaskofu wanapaswa kuimarisha maono hayo ya waasisi hususani mada saba za mkutano Mkuu wa Kwanza wa AMECEA Julai 1961.
Katika mkutano huo Mkuu wa kwanza wa AMECEA, baadhi ya mada zilikuwa ;Kanisa na Vyombo vya habari kwamba Maaskofu waanzishe kituo cha televisheni cha AMECEA, radio ya AMECEA na kiwanda cha uchapichaji cha ukanda huo.
Pawe na kituo cha kutoa malezi ya kiroho kwa mapadri wa jimbo, Chuo Kikuu cha Ukanda ambapo  tayari  kipo chuo Kikuu cha Afrika Mashariki CUEA, masuala mbalimbbali ya haki na amani nk.
Huku wakiendelea kutathmini hayo wanapaswa kujua kuwa, ingawa AMECEA ina mafanikio bado kuna changamoto mbalimbali zinazopaswa kutatuliwa kwa ajili ya maendeleo ya nchi wanachama wa AMECEA.
Aidha wakumbuke kuwa, wafadhli wamepungua hivyo maaskofu wanapaswa kuwa na mbinu za kujitegemea ili asilimia kubwa ya mapato yao yatokane na mapato ya ndani badala ya nje.
Ndiyo maana Missio kwa kushirikiana na AMECEA na TEC wanatoa mafunzo hayo yakini ili maaskofu  wapate ujuzi na mbinu za kubuni miradi ya kujitegemea ikiwemo kubuni miradi endelevu.
Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Padri Dkt. Charles Kitima amesema kuwa, mkutano huo unakuja wakati Kanisa linapaswa kupata mbinu na ujuzi wa kumiliki rasilimali watu, fedha  nk. ambazo ni endelevu.
Ametaka  washiriki watathmini ni kwa jinsi gani wana mikakati endelevu ya Usimamizi wa taasisi, Uongozi Endelevu; Umoja wa Kanisa Katoliki, Ushauri na Usimamizi.
 “Hatuwezi pia kufanikiwa katika hayo bila ya kuwa na umoja na mshikamano.  Mafanikio ni kuwa na uongozi bora unaotoa miongozo yenye tija na ushirikiano na mikakati endelevu ya maendeleo,” amesema Padri Kitima.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU