Dkt. Kikwete hatalisahau Kanisa Katoliki-Ridhiwani














Na Pascal Mwanache
LIKIELEKEA katika kufanya kilele cha Jubilei ya miaka 150 ya Uinjilishaji Tanzania Bara hapo Novemba 4, 2018, imeelezwa kuwa uwepo wa Kanisa Katoliki nchini na ujio wa wamisionari umekuwa mkombozi wa watanzania hasa katika sekta ya elimu na afya, ambapo familia ya Rais Mstaafu wa awamu ya nne Dkt. Jakaya Mrisho Kikwete imeweka wazi kuwa haitalisahau Kanisa Katoliki.
Hayo yameelezwa na Mbunge wa Chalinze na mtoto wa Dkt. Kikwete, Ridhiwani Kikwete, wakati akiongea na waamini wa Parokia ya Bikira Maria Mama wa Kanisa Kigurunyembe Jimbo Katoliki Morogoro, wakati wa Misa Takatifu ya Kutabaruku Kanisa hilo.
“Babu yangu mzee Mrisho Kikwete, ambaye kwa ufundi na utaalamu wake alioupata katika Kanisa Katoliki, hata walipokuja watawala wa kijerumani walimuona anafaa kuwa mmoja wa viongozi. Akachaguliwa kuwa wakili wa wajerumani katika shughuli zao pwani ya Afrika Mashariki, hata baadaye wanawe wakasoma katika mfumo huo huo hata wajukuu wake. Kwa mfano Jakaya Kikwete ambaye ni baba yangu mimi, amesoma Middle School katika shule ambayo kipindi hicho ilikua inaitwa Lugoba ambayo inaendeshwa na Kanisa Katoliki mpaka leo hii. Kwa hiyo Kanisa Katoliki lina mchango mkubwa katika familia yangu” ameeleza Ridhiwani.
Akielezea historia ya kuingia kwa ukristo nchini, Ridhiwani amesema kuwa Bagamoyo ina historia kubwa katika Tanzania kwa kuwa historia ya Kanisa Katoliki inaanza na historia ya ujio wa wamisionari waliotokea Re-union na kisha kufika Zanziba na baadaye wakavuka maji hadi Bagamoyo walikousimika msalaba.
“Tokea kipindi hicho kwa ushuhuda kabisa tumeendelea kuneemeka kwa Kanisa Katoliki katika nyanja mbalimbali. Mimi mwenyewe katika historia ya maisha yetu, ni moja kati ya familia zinazosimama mbele yenu hapa kutoa shukrani zangu kwa Kanisa Katoliki”. Amesema.
Akitoa homilia yake katika Misa hiyo Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amesema kuwa utakatifu wa kanisa ni lazima utokane na wa waamini hivyo kuwataka waamini wa Parokia hiyo kujitakasa ili matumizi ya kanisa hilo yalete maana kusudiwa.
“Jengo hili litakuwa tu takatifu kulingana na utakatifu wa mwenendo wenu. Mkilitumia kwa matumizi tofauti mtakuwa mmekufuru. Hivyo basi, kanisa hili litakuwa na maana kutokana na sisi waamini tunaoingia hapa” amesema Kardinali Pengo.
Kanisa hilo la Parokia ya Kigurunyembe limetabarukiwa na Kardinali Pengo na limetumia takribani miaka 10 hadi kukamilika kwake ambapo mwaka 2013 Dkt. Kikwete aliongoza harambee ya ujenzi wa Kanisa hilo iliyofanikisha kupatikana kwa Tsh. Milioni 200, huku Dkt. Kikwete akichangia Milioni 70.


Comments

  1. Asante Mungu kwa kufanikisha kutabarukiwa kwa kanisa letu la Bikira Maria Mama wa Kanisa.

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU