Wanaosimamia watoto katika ubatizo wawe waamini waliokomaa kiimani-Ask. Rwoma


Mapadri, wazazi na viongozi wa Kanisa wametakiwa kuwa makini kuwachagua wasimamizi wenye uelewa na Imani, na kuwaonyesha njia wale wote wanaowasimamia  watoto katika Sakramenti mbali mbali za Kanisa Katoliki.
Wito huo umetolewa na Askofu wa Jimbo Katoliki Bukoba Mhashamu Desderius Rwoma katika homilia yake wakati wa Misa Takatifu ya somo wa Parokia ya Mt. John Bosco katika Parokia ya Mt. Yohani Bosco - Kamishango Jimboni humo.
Katika homilia yake Askofu Rwoma amesema kuwa, ni vizuri wazazi wakawachagulia watoto wao wasimamizi wenye sifa na waliokomaa kiimani katika Sakramenti za ubatizo na kipaimara.
''Katika Sakramenti za Kanisa kuna mtu anaitwa msimamizi, sasa sifa kuu ya msimamizi ni kumuonyesha njia yule unayemsimamia, mzazi anapaswa kuwa kiongozi kwa yule unaye msimamia na kiasi cha maisha anayoishi unaweza kusema huyu anaweza kuwa mtu mwema sio kuokota okota tu mtaani.
Aidha, anayekuwa msimamizi lazima amjue vyema anayemsimamia ili  kumshauri asije akapotea njia na kuingia kusiko faa, sasa unadhani msimamizi akiwa mlevi muda wote yupo kwenye pombe ataweza kumshauri na kumkea aliyepokea sakramenti,'' amesema Askofu Rwoma.
Aidha Askofu Rwoma amewataka  Wakristo wakatoliki kuzitumia vizuri karama za upendo na huruma walizopewa na Mungu, na kuzionyesha kwa wengine, na kutanguliza karama ya sala kuwa kipaumbele  kwa kila jambo. 
''Karama ya huruma na upendo kila mmoja amepewa, onyesheni karama hizo kwa wengine pamoja na karama ya sala ambayo ni karama za kila mtu.
Kila mmoja anatakiwa kusali yeye na familia yake na kusali pamoja na wengine, hivyo ni vizuri mkazionyesha karama hizo na kuwashirirkisha wengine na tutangulize kilicho cha kwanza ambayo ni sala, '' amesema Askofu Rwoma.
Pia amezitka jumuiya ndogo ndogo kusali pamoja ili kujiiimarisha kiroho katika kutafuta utakatifu na kuwa marafiki kwa   wakosefu ili kuwarudisha katika njia inayofaa kama alivyofanya Mt. Yohani Bosco na kusaidiana katika shida mbali mbali. 


Katika Misa hiyo Takatifu, Askofu Rwoma wametoa Sakramenti ya ubatizo kwa watoto zaidi ya 325 na kusimika jumuiya ndogo ndogo zaidi ya 70, amewabariki waamini waliorudi katika sakramenti mbali mbali za Kanisa pamoja na kuwaapisha viongozi wa vyama vya kitume, jumuiya ndogo ndogo na viongozi wa Halmashauri ya Parokia.. 

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU