Askofu Amani awapongeza watawa wa Shirika jipya Arusha walioweka nadhiri




ASKOFU Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki  Arusha Mha. Isaac Amani, ameitaka jamii kuwa tayari na kufanya maandalizi ya kina katika kuitikia na kuuchuchumilia wito wowote wa maisha wa kuwatumikia watu kadri ya mpango wake  Mungu Mwenyezi.
Rai hiyo ameitoa mwishoni mwa wiki jimboni humo akiihubiria hadhira ya waamini waliofurika katika Kanisa la Mt. Yokobo Mtume Parokiani Moshono kwenye sherehe za kuweka nadhiri za kwanza za kitawa kwa masista watatu wa kwanza wa Shirika jipya la Kimisionari la Ekaristi Takatifu na Uinjilishaji Mpya.
Askofu Mkuu Amani amefafanua kuwa wito uwe wa maisha mathalani;  ndoa, utawa na upadri au wa kitaaluma na wa kiuongozi chimbuko lake ni Mwenyezi Mungu mweyewe anaeanzisha na kumwita mtu kutumika ipasavyo na wala si kutumikiwa. “Mwenye kuita ni Mungu na mwenye kuitwa ana kazi tatu kuu, mosi kuisikia sauti ya Mungu, pili kuitikia kwa kuikubali na kuishi agizo la Mungu na tatu ni  kufikisha ujumbe wa Mungu kwa watu kwa ajili ya maendeleo yao ya kiroho, kimwili na kijamii”,  amesema Askofu Mkuu Isaac Amani.
Akiwapongeza na kuwaasa masista watatu walioweka nadhiri hizo za kwanza za maisha ya kitawa ambazo ni usafi wa moyo, ufukara na utii, Askofu Mkuu Amani amesema, “ Wanangu Masista Dafrosa Neema Shayo kutoka Jimbo la Moshi, Daria Markus Ndaligwa kutoka Jimbo la Iringa na Monika Godfrey Mdoe kutoka Jimbo la Tanga, nawapongeza sana kwa kuitikia wito huu wa kuwa wachumba wa Bwana wetu Yesu Kristo, nawasihi sana msiangalie nyuma na kuwaza habari ya kuchagua wito mwingine, endeleni kuisikia sauti yake Kristo ndani yenu, mkiishi kiaminifu nadhiri zenu katika kumtumikia Mungu na watu wake, na sanjari na hilo nawapongeza pia wazazi kwa kuwatoa watoto wenu kwa Kanisa, sasa wasaidieni na wala msiwe kikwaza kwao mathalan kuanza kuwaomba wawasaidie kiuchumi au kuwatafutia ufadhili wa kusomesha wadogo zao.”
Kwa upande wa mwanzilishi wa Shirika la Masista Wamisionari wa Ekaristi Takatifu na Uinjilishaji Mpya Sr. Gisela Upendo, akionesha furaha na shukrani kwa Mwenyezi Mungu amesema, “ hakika kwa unyenyekevu mkubwa namtukuza Mungu nikijawa shukrani za dhati kwake na kwa Uongozi Hairakia wa Kanisa letu, Serekali ya Nchi yetu,  sanjari na watu mbalimbali ambao kwa sala, nia njema, shime na misaada mbalimbali leo hii tunashuhudia matendo haya makuu ya Mungu, kwao wote, tunawaahidi sala zetu kwani hatuna zaidi cha kuwapa.”
Mbali na utume wa kufundisha dini mashuleni, kutembelea wagonjwa na kushiriki sala za Jumuiya Ndogo Ndogo, Shirika hili changa kabisa jimboni Arusha, kwa kipindi kifupi cha takribani miaka mitano tangu kuanziswa kwake, kupitia wafadhili kutoka Bolzano Italia  limefanikiwa kujibu kero ya  jamii ya maji safi na salama kwa kuchimba na kusambaza maji ya kisima kwa shule nne za serikali na kwa jamii kubwa ya Kata ya  Baraa Moshono.
Na kwa sasa Shirika hilo kupitia ufadhili kutoka taasisi ya Circle Association for Cooperation and Development  linajenga chuo cha ufundi mbalimbali kwa ajili ya vijana wa familia masikini ili kuwawezesha kujiajiri mara baada ya kufuzu masomo yao. Ujenzi huo kwa sasa umefikia hatua ya lenta na ukikamilika chuo kitakuwa na uwezo wa kuwa na vijana mia mbili.

Shirika la Masista Wamisionari wa Ekaristi Takatifu na Uinjilishaji Mpya lilianzishwa Jimboni Arusha  kwa ruhusa ya Askofu Mstaafu Josaphat Lebulu baada ya taratibu zote za Kikanisa kukamilika huko Roma Italia na limesajiliwa na Serikali Nchini. Kwa sasa chini ya uongozi wa Mwanzilishi wake ambae ni Mtanzania wa kutoka Jimbo Katoliki Same Sr. Gisela Upendo, shirika lina idadi ya walelewa 23,Wanovis 3,Wapostolant 7,Wakandidat 13 na  masista 3 ambao mwishoni mwa wiki waliweka nadhiri zao za kwanza na kufikisha idadi ya Masister kuwa 4. 

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU