Msitumie vibaya utajiri wenu -Askofu Kinyaiya asema


Na Ndahani Lugunya na Rodrick Minja, Dodoma

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki Dodoma Mhashamu Beatus Kinyaiya, amekemea tabia ya baadhi ya wakristo waliopewa utajiri na Mwenyezi Mungu kuutumia vibaya utajiri huo hususani kwa kuwanyanyasa wanyonge, yatima, masikini na wasiojiweza.

Ameyasema hayo wakati akitoa homilia yake kwenye adhimisho la sadaka ya Misa Takatifu, katika Parokia ya Bikira Maria Mama wa Damu Azizi ya Yesu-Kisasa Jimboni Dodoma, Misa iliyokwenda sambamba na utoaji wa sakramenti Takatifu ya kipaimara kwa vijana 76 wa Parokia hiyo.

Katika homilia yake Askofu Kinyaiya amesema kuna baadhi ya wakristo wamejaliwa kupata utajiri kwa halali kabisa, lakini kosa linakuja pale mtu anapoutumia utajiri huo kwa ubadhilifu na kuzitumia katika matumizi yake ya kila siku pasi na mpangilio mzuri.

“Mmejaliwa utajiri na Mwenyezi Mungu hivyo utumieni kwa kutenda mema na sio kunyanyasa wengine ambao hawakujaliwa utajiri huo kwani hata ipo siku mwenyezi munghu anaweza kukunyang`anya utajiri huo pasi kujua lolote lile” aliongeza Askofu Mkuu Kinyaiya
  
Katika hatua nyingine  Askofu Kinyaiya amewataka wazazi na walezi wenye watoto kuanzia umri wa mwaka mmoja hadi miaka saba, kuanza kuwajengea msingi wa kuwafundisha lugha ya kiingereza kabla ya kuwapeleka shuleni kuanza elimu ya msingi.

Amesema kwamba, umri wa mtoto kuanzia miaka hiyo akili yake ni kama sponji mpya ambapo huwa ni mwepesi wa kufyonza kila kitu kwenye akili yake, kumbe wazazi wenye watoto wa umri huo wawafundishe lugha ya kingereza kabla hawajawapeleka shuleni.

“Kwahio  sasa wazazi wenye watoto wadogo, umri wa kumsaidia mtoto ni pale anapokuwa kuanzia mwaka wa kwanza mpaka wasaba akili yake kama sponchi mpya inayofyonza kila kitu, na ndio maana watoto wanakuwa wepesi sana ukimnyima kitabu ataokota hata karatasi njiani atasoma, akili ina dai ina uwezo mkubwa,’ amesema.



Amesema moja ya tatizo lililopo nchini kwa watoto kutokufanya vizuri katika elimu ya sekondari ni lugha ya kingereza, kwani wanapokuwa katika elimu ya msingi wanafundishwa masomo yao kwa kutumia lugha ya Kiswahili, hivyo wanapofika ngazi ya sekondari lugha ya kiingereza inawapa shida.

Sasa wazazi tunawasaidiaje katika hilo, kama tumeshajua ile miaka saba ndio mahali pazuri kwa mtoto kufyonza, wazazi muanze kusaidia watoto wakiwa nyumbani bado kwenye suala la lugha,” amesema Askofu Mkuu Kinyaiya.

Ameongeza na kusema kwamba  wazazi wasisubiri tu watoto wakafundishwe lugha ya kingereza wakiwa shuleni, wakati wapo watu wa karibu nyumbani wanaoweza kuwafundisha lugha hiyo wakiwa hapo, ambapo amesema kama yupo Baba, Mama, Kaka au Dada anaejua kingereza basi awajibike kumfundisha mtoto.

Katika hatua nyingine amewataka vijana walioimarishwa kwa sakramenti ya Kipaimara na vijana wengine  nchini, kujiepusha na makundi mabaya yanayojihusisha na utumiaji wa bangi na madawa mengine ya kulevya.

Amesema mazingira mtu anayoishi wakati mwingine yanaweza kumfanya mtu akawa hovyo asipokuwa mwangalifu, hivyo akawataka vijana kujitahadharisha na marafiki wanaoweza kuwashawishi kutumia madawa ya kulevya.

Amewataka waimarishwa hao kusimama imara katika kuitetea imani ya Kanisa Katoliki popote pale wanapkuwa, kwani tayari wamekwishakuwa watu wazima kiimani.


Ibada hiyo ya Misa Takatif imekwenda sambamba na zoezi la kubariki jiwe la msingi la ujenzi wa Kanisa la parokia hiyo, ambapo ujenzi huo umefikia hatua ya kunyanyua nondo na umekwisha gharimu takribani milioni 200 mpaka sasa.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU