Jubilei miaka 75 Masista wa Upendo

‘Mkiushinda ubinafsi mtafanikiwa’


Na Pascal Mwanache, Mbingu
MASISTA wa Shirika la Upendo wa Mt. Fransisko Mahenge wameaswa kufanya kazi kwa kushirikiana huku wakiweka kando ubinafsi ili kazi zao ziendelee kumtukuza Mungu.
Hayo yameelezwa na Askofu wa Jimbo Katoliki Tundu-Masasi Mhashamu Filbert Mhasi katika Misa Takatifu ya kuwakumbuka marehemu waanzilishi wa shirika hilo la masista pamoja na masista waliofariki, ikiwa ni sehemu ya sherehe ya jubilei ya miaka 75 ya shirika la masista wa upendo wa Mt. Fransisko Mahenge.

Akitoa homilia katika misa hiyo Askofu Mhasi amewaasa masista hao kutotafuta mtetezi mwingine zaidi ya Mungu pale wanapokabiliwa na changamoto mbalimbali katika utume wao, bali wadumu katika uthabiti wa imani yao na Mungu atawatetea.
“Inatupasa kumshukuru Mungu kwa imani tuliyojaliwa kupitia Kristo. Waanzilishi wa shirika hili walipigana vita vizuri na waliamini kuwa kuna maisha baada ya kifo. Ndiyo maana wakawa imara katika imani yao. Hawakuwa wabinafsi, nanyi hamna budi kufanya kazi kama timu huku mkiweka ubinafsi pembeni” ameeleza Askofu Mhasi.
Kwa upande wake Askofu wa Jimbo Katoliki Ifakara Mhashamu Salutaris Libena amewataka masista hao kuendelea na jitihada za kumkomboa mwanadamu kimwili na kiroho kama walivyofanya watangulizi wao.
Ameyasema hayo katika adhimisho la Misa Takatifu ya kutangaza injili iliyofanyika Oktoba 3, 2019 kuelekea kilele cha jubilei ya miaka 75 ya Shirika la Masista wa Upendo wa Mt. Fransisko Mahenge.
Akitoa homilia katika misa hiyo Askofu Libena amewaomba watawa hao kuendelea kuhubiri kwa maisha na matendo yao kwa kumkomboa mwanadamu mzima kiroho na kimwili kupitia utume na huduma mbalimbali za kijamii.
“Mfanye yale ambayo wale waliokuja kutangaza Injili waliyafanya. Imani tuliyoirithi kutoka kwao tuirithishe kwa wengine ili wamjue Mungu kwani dunia ina kiu ya neno la Mungu. Wengi bado hawajamjua Mungu hivyo twende tukawainjilishe” ameeleza Askofu Libena.

Kardinali Pengo aagwa na kupongezwa Ifakara
Awali katika hatua nyingine waamini wa Jimbo Katoliki Ifakara wameungana katika adhimisho la Misa Takatifu kwa ajili ya kumpongeza Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo kwa kutimiza miaka 75 ya kuzaliwa.
Akitoa neno la shukrani katika misa hiyo Kardinali Pengo ameeleza kuwa amefurahi kuona jimbo hilo halijadumaa bali linaendelea kukomaa.
“Jimbo la Dar es salaam limezaa jimbo la Mahenge na Jimbo la Mahenge limezaa jimbo hili la Ifakara. Kwa hiyo ninafurahi kuwaona wana Ifakara ambao ni wajukuu wa jimbo la Dar es salaam. Nafurahi mmebaki wema na hamjadumaa” ameeleza.
Shirika la Masista wa Upendo wa Mt. Fransisko wa Asizi lilianzishwa Juni 8, 1941 na Askofu Mkuu Edgar Maranta OFMCap katika Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam. Wakati huo jimbo la Mahenge lilikuwa sehemu ya Jimbo Kuu la Dar es salaam ambapo wakati huo Askofu Mkuu Maranta alikuwa Askofu Mkuu wa Dar es salaam.

Idadi ya wanashirika iliyopo sasa ni 334 ambapo masista wenye nadhiri mi 268 na walelewa wapatao 66.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU