Jamii yatakiwa kuthamini wazee

Jimmy Mahundi, Mtwara
Jamii imetakiwa kuacha tabia ya kuwatelekeza wazee na kuwaacha waishi katika mazingira magumu.
Kauli hiyo imetolewa na wazee walioshiriki kongamano la wazee katika kuadhimisha siku ya wazee duniani ambapo kitaifa imefanyika mkoani Mtwara na kuhudhuliwa na wawakilishi wa wazee kutoka mikoa mbalimbali hapa nchini.
Wazee hao wamedai kuwa kwa sasa wengi wao wanaishi maisha magumu sana kutokana na vijana wao waliowasomesha kwa shida na taabu leo wanawaona mizigo na wanashindwa kuwasaidia.
“Baadhi ya watoto wetu wanatuona kama mizigo maana hatuna nguvu tunawategemea kwa kila kitu.
Pia wanasahau kutimiza wajibu wao wa kulea  wazazi wao kama sisi tulivyotimiza wajibu wetu kuwalea na kuwasomesha.
Hivyo wanaposahau kuwa nasi pia tuliwalea na kuwapa elimu, wanajiona kuwa  mafanikio wanayopata ni kutokana na juhudi zao tu.
Inasikitisha kuona wazee  wanaishi maisha magumu sana kwa kuwa watoto wao wanawaona kuwa ni mizigo isiyobebeka”amesema Mzee Mohamedi Selemani.
Miongoni mwa changamoto ambazo zinawakabili wazee kwa sasa katika maeneo mengi ni pamoja na huduma za afya,ambapo wameiomba serikali kuendelea kuboresha sera ya afya ambapo itakuwa msaada kwa wazee ambao walitumia muda na nguvu zao katika kulitumikia taifa.
Pia wazee wametakiwa kushikamana ili kujikwamua katika uzee wao ambapo ni umoja wao pekee ndio utasaidia kufikisha vilio vyao kwa serikali na jamii kwa ujumla maana bado kuna kundi kubwa la wazee ambao wameendelea kuwa nje ya umoja hali ambayo inachangia kushindwa kujua changamoto zinazowakabili.
Aidha pia vijana na viongozi katika nafasi mbalimbali wametakiwa kuwakumbuka na kuwajali wazee kwa kuwa wao ni sehemu muhimu ya ustawi wa taifa na maisha ya watanzania na wamekuwa historia katika harakati mbalimbali za uhuru na maendeleo ya taifa.
 Wanapozeeka jamii inayo wajibu wa kuwaenzi kwa kazi zao zilizotukuka.
Akifungua kongamano la wazee kitaifa  lililofanyika katika ukumbi wa Benki Kuu Kanda ya Kusini Mtwara, Katibu Mkuu Wizara ya Afya Maendeleo ya Jamii Jinsia na Watoto, Idara Kuu ya Maendeleo ya Jamii Dakta John Jingu, amedai kuwa chimbuko la siku ya wazee duniani ni azimio la umoja wa mataifa namba 45/2006  la mwaka 1990  na kuwataka mataifa kuwaenzi wazee wote duniani na kuwajali pamoja na kuboresha maisha yao.
Katika kongamano hilo Katibu huyo Mkuu amewataka wazee washiriki wa kongamano hilo kujikita pia katika kutoa maoni juu ya nini kifanyike katika kuwahudumia wazee na kuboresha maisha yao baada ya kulitumikia taifa katika nafasi mbalimbali kwa kutoa mapendekezo yatakayosaidia  kuboresha sera ya wazee.
Aidha amedai kwa sasa serikali inafanya mapitio ya sera ya wazee na ametaka kongamano hilo kuwa sehemu ya maoni ambayo yatasaidia kuboresha kwa kuwa washiriki wengi wamatoka katika maeneo mbalimbali ya nchi hivyo kwa sasa ipo katika hatua ya kukusanya maoni toka kwa wananchi na wazee wenyewe.
Katika kongamano hilo miongoni mwa maoni ambayo wazee wameyatoa ni pamoja na kuiomba serikali kuwawekea dawa zinazoendana na magonja ya wazee kwa kuwa kwa sasa katika hospitali nyingi nchini zina ukosefu wa dawa kwa wazee hali ambayo inachangia vifo visivyotarajiwa.
“Tunaiomba serikali iangalie suala la madawa yanayoendana na magonjwa ya wazee kwakuwa mara nyingi tunakosa dawa mahospitalini na kusababisha vifo vya wazee hapa nchini kuongezeka,”amesema Hafsa Kiyasile.
Pia kuhusu suala la wazee kuondolewa katika makundi maalum ambayo yananufaika na mambo mbalimbali kama vile mikopo,jambo hilo linaleta simanzi kwao na wameitaka serikali kuwaweka kama yalivyo makundi ya wanawake,vijana na walemavu ili nao wastahili mikopo kama haya makundi yanavyonufaika.

Wamependekeza wazee wapewe pensheni kila mwezi kama ilivyo Zanzibar .

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU