TEC yawataka watunzi wa nyimbo za Kanisa kuzingatia miongozo ya Kanisa

Na Dalphina Rubyema, Dar es Salaam
KANISA Katoliki nchini limezidi kuwasisitiza watungaji na waimbaji wa muziki wa Kikatoliki kuzingatia misingi na miongozo ya Kanisa hilo badala kuiga mitindo na mahadhi ya  madhehebu mengine.
Rai hiyo imetolewa na Mwenyekiti wa Idara ya Liturujia ya Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania (TEC), Mhashamu Salutaris Libena, katika mahojiano maalum  na KIONGOZI, muda mfupi baada ya kufunga mkutano wa mwaka wa Liturujia Taifa, uliofanyika jijini Dar es Salaam na kuwashirikisha wajumbe wa Kamati ya Muziki kutoka Kanda za Kanisa Katoliki nchini, Waratibu wa Liturujia wa Majimbo, Walimu wa Liturujia katika Seminari Kuu na baadhi ya vyuo vya Makatekista nchini.
Amesema kuwa kama inavyosisitizwa kwenye Katiba ya Utume wa Kwaya Katoliki Tanzania (UKWAKATA), mtindo uimbaji ukiwemo utoaji wa sauti katika muziki Mtakatifu wa Kanisa hilo, haunabudi kuwa wa kiasili au kibantu na siyo wa kuiga mahadhi ya nje ama ya madhehebu mengine.
“Waimbaji waepuke kuwa kikundi cha burudani kwa kufuata matendo na mkao wa waamini wote katika maadhimisho ya Liturujia…nyimbo zenye mahadhi ya kidunia zisitumike katika maadhimisho ya Kiluturujia kwani hazifadhili dhana ya kuimba vizuri ni kusali mara mbili,” alisisitiza.
Mintarafu  mkutano huo ulioandaliwa na ofisi ya Idara ya Liturujia ya TEC, Mhahsamu Libena alisema ulilenga  kujadili na kuangalia maendeleo ya Liturujia katika majimbo ya Kanisa Katoliki nchini pamoja na kupata mrejesho wa utunzi na uimbaji wa muziki Mtakatifu, kwa kuzingatia Katiba ya UKWAKATA ambayo ilianza kutumika rasmi Desemba 2 mwaka jana yaani Jumapili ya kwanza ya Majirio.
Alisema kutokana na mrejesho uliotolewa na washiriki wa mkutano huo kutoka majimbo mbalimbali, unaonesha kuwa waliofuata katiba hiyo kikamilifu imeleta mafaniko hasa kwa kuwapata wanakwaya sahihi wanaofuata kanuni na misingi ya Kanisa Katoliki hasa suala la ushiriki wa jumuiya ndogondogo za Kikiristo.
“UKWAKATA katika ukurasa wake wa 40 ina fomu maalum inayomtaka mwanakwaya kujaza na ina vipengele mbalimbali kikiwemo kile cha kufahamika jumuiya anakotoka… kwa kweli waliyoizingatia kikamilifu wameonesha mafanikio makubwa, “ alisema.
Hata hivyo alikiri kuwa baadhi ya vipengele vya Katiba hiyo havijafahamika vilivyo, hivyo akatoa rai kwa waratibu wa Liturujia majimboni kutoa elimu na ufafanuzi kwa wadau wa muziki Mtakatifu wakiwemo watunzi na wanakwaya ili viweze kueleweka.
Sanjari na hayo, Mhashamu Libena ambaye pia ni Askofu wa Jimbo Katoliki la Ifakara alisema, licha ya Kanisa Katoliki kuheshimu Teknolojia ya Mawasiliano, lakini katu halitaruhusu waamini wake kutumia simu za mikononi  na vifaa vingine vya namna hiyo, kama sehemu ya kufanyia rejea wakati wa Misa na Ibada Takatifu.
“Tunaendelea kutumia Biblia Takatifu na maandiko mengine yaliyochapishwa kwa kuidhinishwa na Kanisa ambayo tayari yamo katika maandishi yaliyochapishwa… siyo kuruhusu simu, ipad na vifaa vingine vya namna hiyo,” amesema.
Akizungumzia msimamo wa Kanisa hilo, Bw. Benjamin Mshana mwamini wa Parokia Katoliki ya Kibwegere Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, ameunga mkono msimamo huo wa Kanisa kwa kile alichoeleza kuwa kuruhusu matumizi ya simu wakati wa Misa ni sawa na kumruhusu shetani ambaye bila shaka atawafanya waamini hao wakose utulivu wakati wa adhimisho la Misa Takatifu

“Unakuta mtu anafungua simu na anakutana na ujumbe, ni wazi kwamba shetani naye atachukua nafasi yake kwani hawezi kuacha kusoma ujumbe huo na tayari utulivu wake kanisani unakuwa wa mashaka,” amesema Bw. Benjamin.

Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU