Ukuaji uchumi usioheshimu mazingira ni uasi-Ask. Banzi


Na Pascal Mwanache, Korogwe
IMEELEZWA kuwa uharibifu wa mazingira unaofanywa kwa jina la maendeleo na ukuaji wa uchumi ni uasi sawa na kuabudu miungu, huku wito ukitolewa kwa kila mwanadamu kusheshimu kazi ya uumbaji.
Hayo yamesemwa na Askofu wa Jimbo Katoliki Tanga Mhashamu Antony Banzi katika Misa Takatifu ya kuwasimika viongozi wapya wa Shirika la Masista wa mama yetu wa Usambara (COLU) iliyofanyika katika Makao Makuu ya shirika hilo huko Kwamndolwa, Korogwe.
Akitoa homilia yake katika misa hiyo Askofu Banzi amesema kuwa mwanadamu amepewa mamlaka juu ya mazingira huku akitakiwa kutumia zawadi ya akili na utashi katika kuutiisha ulimwengu na vilivyomo kwa manufaa ya leo na kesho.
“Kuiheshimu dunia ni moja ya maadili na ni amri ya Mungu. Kuharibu mazingira ni kuabudu miungu. Tusiitumie dunia kwa fujo kwani atakayeathirika ni mwanadamu mwenyewe. Tukiitunza nayo itatutunza” amesema Askofu Banzi.
Pia ametaka kuwepo kwa njia rafiki katika uvuvi na ufugaji wa nyuki, huku akikemea matumizi ya mabomu na nyavu zisizofaa katika shughuli ya uvuvi, sambamba na uchomaji wa nyuki wakati wa kurina asali, akisema kuwa njia hizo zinapelekea uharibifu mkubwa wa mazingira.
Aidha Askofu Banzi ameweka wazi kuwa matatizo mengi yanayotokea katika jamii husababishwa na kukosa mahusiano mazuri kati ya mwanadamu na Mungu, ambapo ametaja mwarobaini wa uharibifu wa mazingira kuwa ni mahusiano mazuri na Mungu pamoja na kuwa na sheria ambazo msingi wake ni Mungu.
“Tunaiharibu dunia kwa sababu hatuna mahusiano mazuri na Mungu, hatuna mahusiano mazuri katika jamii zetu na hata familia zetu” amebainisha.
Wakati huo huo ametoa rai kwa waamini kutofikiria suala la talaka na badala yake ametaja dawa ya changamoto za ndoa kuwa ni kujenga mahusiano mazuri na Mungu.
“Talaka ni matokeo ya kukosa mahusiano mazuri na Mungu. Ukiona mtu anang’ang’ania jambo hilo daima huwa ni kwa sababu ya ugumu wa mioyo, jambo la muhimu ni kubaki katika ndoa ama wito wa utawa” ameongeza.

Uongozi mpya wa COLU wasimikwa
Katika hatua nyingine Askofu Banzi amewasimika rasmi viongozi wa Shirika la Masista wa Mama yetu wa Usambara (COLU) ambapo Mama Mkuu aliyechaguliwa kuongoza masista hao ni Sista Maria Gaspara Kashamba, ambaye amechaguliwa kwa awamu ya pili mara baada ya kuwa Mama Mkuu kwa miaka sita iliyopita.
Wengine ni Sista Maria Focus Mjema aliyechaguliwa kuwa Mama Mkuu msaidizi, Sista Maria Regina, Sista Maria Vincent na Sista Maria Eveta. Viongozi hao wamekula kiapo mbele ya Askofu Banzi na waamini waliohudhuria misa hiyo.
Askofu Banzi amesema kuwa kazi ya Mama Mkuu huyo mpya ni kumiliki, kulinda na kuendeleza utume na amali zote za shirika hilo hasa kwa kumtanguliza Mungu.

Lijue Shirika la COLU
Shirika la Masista wa Mama yetu wa Usambara (COLU) lilianzishwa mwaka 1954 katika mkoa wa Tanga kwenye milima ya Usambara katika Wilaya ya Lushoto na aliyeanzisha shirika ni Monsinyori Eugeni Arthurs wa Shirika la Mapendo (Mapadri Warosmini).
Monsinyori aliomba Masista wa Damu Takatifu (CPS) ili walilee shirika hili jipya, ndipo apopewa Sista Wilibalda Giesbers akishirikiana na Sista Ambrose Mollers ambao walilea na kuliongoza shirika tangu mwaka huo wa 1954 mpka 1976 walipopokelewa na Sista Inviolata Mndeme, Mama Mkuu wa kwanza mzalendo.
Walezi hawa waliwapokea wasichana 12 mwaka 1954 katika shirika. Hadi leo bado wapo masista wawili waliobaki baada ya wenzao kufariki dunia, nao ni Sista Ancilla Macha na Sista Bernadetha Massawe.
Shirika hili limekuwa na watawa wake wafanyakazi katika majimbo ya Tanga, Moshi, Dar es salaam, Same, Mbulu na Reggio Calabria Italia, ambapo wanatoa huduma za kufundisha dini maparokiani, kufundisha kwenye shule za chekechea, msingi, sekondari na vyuo. Pia wanawahudumia wagonjwa mahospitalini,vituo vya afya, zahanati na majumbani.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU