Balozi wa Papa apongeza Kanisa katika mapambano dhidi ya mila potofu




Na Veronica Modest, Serengeti
BALOZI wa Baba Mtakatifu nchini Askofu Mkuu Marek Solczynski  amelishukuru Kanisa Katoliki kwa kuendelea kutoa elimu juu ya madhara ya mila potofu, hasa ukeketaji wa watoto wa kike, ndoa za utotoni na ndoa za mitara.
Akizungumza na Kiongozi mara baada ya kuhitimisha ziara yake ya kichungaji  ya siku 8 ndani ya Jimbo Katoliki Musoma balozi huyo amesema kuwa, kuna baadhi ya  udekano alizotembelea  na amekutana na changamoto kubwa ya kupewa taarifa ya kuwepo kwa vitendo vya ukeketaji wa watoto wa kike, ndoa za utotoni na ndoa za mitara ambazo zimekuwa changamoto kubwa kwa wakristo walio wengi hata kushindwa kupata sakramenti takatifu ya ndoa kutokana na kuwa na wake wengi.
“Nimefika nimeona mimi mwenyewe kwa macho yangu ,nimesikia kutoka katika taarifa zilizowasilishwa kwangu na mapadri wa udekano wa Tarime, Rorya na Serengeti. Awali nilikuwa nasoma kwenye vyombo vya habari ila nimewaona na waamini wetu hivyo ninalishukuru kanisa kwa kuendelea kupambana na changamoto hizi na Mungu atawasaidia na sisi tunazidi kuwaombea” amesema balozi huyo.
Naye Askofu wa Jimbo Katoliki Musoma Mhashamu Michael Msonganzila amesema kuwa wanamshukuru balozi wa Papa kwa kutembelea jimbo hilo na kuonana na waaamini sambamba na kujionea changamoto ambazo wanakumbana nazo katika uinjilishaji.
Mkuu wa udekano wa Serengeti ambapo ndipo alipohitimishia ziara yake ya kichungaji na kupata fursa ya kutembelea hifadhi ya wanyama ya Serengeti na kubariki hoteli na waaamini wanaoishi ndani ya hifadhi,Padri Medard Chegere amesema  kuwa ujio wa Balozi huyo umewaimarisha zaidi waamini kiroho, kwani viongozi hao wanapofika  katika maeneo yao ya kichungaji wanawasaidia kuinuka kiimani zaidi.
Padri Chegere amesema kuwa waamini wanapaswa kuishi kwa kufuata mafundisho ya Kristo hivyo kufuata msingi ya imani kutokana na mafundisho ya ubatizo.
Katika hatua nyingine balozi huyo amewaomba  wananchi wa Wilaya ya Tarime kuhakikisha amani upendo na mshikamano uliopo unaendelea kudumu ili kizazi kijacho kiweze kufurahia matunda ya amani hiyo.
Balozi huyo ameyasema hayo alipofanya ziara ya kichungaji katika Parokia ya Tarime na kuweka jiwe na msingi katika ujenzi wa kanisa jipya ambapo alifurahishwa na mapokezi ya viongozi mbalimbali wa dini, serikali na waamini wa parokia hiyo na kusema kuwa ushirikiano huo udumu milele.
“Umoja mliouonyesha ni dhahiri kuwa kuna amani ya kutosha miongoni mwenu, bila kujali itikadi ya dini. Nawaomba ushirikiano huu uendelee hata katika masuala mengine ya maendeleo ndani ya wilaya yenu, ili watoto wadogo hawa watakapokuwa wakubwa waweze kufurahia matunda ya amani hii” amesema Askofu Mkuu Marek.
Kwa upande wake Askofu Msonganzila amesema kuwa Kanisa limekuwa bega kwa bega na serikali katika kuhamasisha umuhimu wa uwepo wa amani miongoni mwao, na hata inapotokea kuna viashiria vya uvunjivu wa amani wamekuwa wakitumia muda mwingi kuhubiri amani na upendo na hata namna ya kupinga mila na desturi potofu,  hususani za ukeketaji kwa watoto wa kike na ukatili wa kijinsia pamoja na nyumba ntobhu ili kudumisha amani.
Mkuu wa Wilaya ya Tarime Glorius Luoga  amesema kuwa kanisa lina mchango mkubwa katika kuhamasisha amani na kwa kudhihirisha hilo ndiyo maana hata katika mapokezi ya balozi kanisa limealika hata viongozi mbalimbali wa madhehebu  mengine hii yote ni kuonyesha ni kwa jinsi gani kanisa lilivyo na ushirikiano.
“Naomba niseme ukweli viongozi hawa wa dini kushiriki katika mapokezi inaonyesha upendo wa kweli kwani wengine wangeweza kukataa, lakini sisi wana Tarime tumekuwa tukifanya kazi kwa kushirikiana pamoja na ndiyo maana amani sasa hivi imetawala, na hata inapotokea dalili za uvunjivu wa amani mimi nikiwa mwenyekiti wa kamati ya ulinzi na usalama tumekuwa tukishirikiana na viongozi wa dini kukemea kwa nguvu zote uvunjifu huo” amesema Luoga.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU