Wanaohitimu elimu ya juu watakiwa kutatua changamoto za wananchi


ASkofu Mkuu Paul Ruzoka wa Jimbo Kuu  Katoliki Tabora amewaasa wahitimu wa Chuo Kikuu Kishiriki cha Askofu Mkuu Mihayo Tabora, (AMUCTA) kutumia elimu waliyoipata katika kutatua matatizo ya wananchi wa Mkoa wa Tabora na Tanzania nzima.
Rai hiyo imetolewa hivi karibuni katika Adhimisho la Misa Takatifu iliyoadhimishwa katika Kanisa la Chuo hicho  ambapo Askofu amesema elimu ina lengo la kumsaidia mwanadamu amudu  mazingira yake .
Elimu ni ufunguo, elimu ni mwanga unaomsaidia mwanadamu kuwa mstaarabu na kupeleka ustaarabu huo kwa wengine katika jamii anayokuwemo na si kitu cha kumpatia mwanadamu kiburi na majivuno.
Askofu Ruzoka amesema, elimu inamsaidia mwanadamu kuwa bora zaidi katika kueleza mambo kwa ufasaha zaidi kwani anakuwa na ufahamu mkubwa zaidi tofauti na hapo awali, elimu hiyo inaongeza ufanisi katika utendaji wake wa kila siku.
Amewataka wahitimu hao kumtanguliza Mungu zaidi ili waweze kutafuta Hekima katika Ukweli, “seek Wisdom in truth” ambayo ndiyo kauli mbiu ya Chuo cha “AMUCTA.”
Tukumbuke kuwa wote tunaingia katika ulimwengu huu na kuondoka kwa namna moja. “Je utakapoondoka utakumbukwa kwa lipi?”. Askofu Mkuu aliuliza.
Aidha Askofu Mkuu Ruzoka amesema kila mhitimu ameiva, hivyo ana kila sifa ya kuwa kiongozi katika jamii ya watu atakaokutana nao, hivyo tumieni elimu mliyoipata kwa faida ya jamii nzima na si kwa maslahi binafsi.
Askofu Mkuu Ruzoka amewasisitiza wahitimu wote kutumia elimu waliyopata kupambanua mema na mabaya.
Aidha Askofu Mkuu Ruzoka amewakumbusha wahitimu wote kuwa na moyo wa shukrani kwa Mungu na wazazi au walezi kwa michango yao mbalimbali iliyowawezesha  kufikia hatua hiyo kubwa katika uwanja wa elimu kwani moyo usio na shukrani hukausha meema yote.
Askofu Mkuu Ruzoka amewasihi wahitimu wote kujiendeleza katika uwanja huo wa elimu ili kwenda sambamba na ulimwengu unaokwenda kasi  hasa katika mabadiliko ya Sayansi na Teknolojia ili wasibaki nyuma ya wakati.
Pia amesema elimu mliyoipata iwaongezee hamu ya kulitumikia Taifa letu na Kanisa zima , daima tukumbuke hapa duniani tunapita na elimu yetu pia na vivuli vyetu, ipo siku itatubidi kutoa hesabu ya maisha yetu, vyema tuishi kwa upendo na watu wote.
Wito ulitolewa pia kwa wanafunzi wote kuweka bidii katika masomo ili kuweza kufikia hatua ya kuhitimu, “komaeni katika kusoma yanawezekana” Askofu Mkuu amesema.
Aidha amesema Digrii mlizopata zitumieni katika kuhudumia watu, nasiyo kupamba katika mitandao ya kijamii bali zitumike katika kuboresha maisha yenu na wengine, mkiwa wabunifu, tayari kujiajiri na kuajiri wengine.
Naye Mkuu wa Mkoa wa Tabora, Aggrey Mwanri akizungumza muda mfupi baada ya Misa Takatifu amewaasa kutumia digri zao kupambana na mazingira na siyo kulalamika kila kunapokucha, jueni kazi ya elimu ni kumpa uwezo mwanadamu kutafuta fursa na kuchukua kadri ya mazingira yake.
Aidha amewaasa wahitimu wote kuwa digrii lazima ilete mabadiliko ya haraka kwa mhitimu mwenyewe na wale wanaomzunguka katika utendaji wake.
Mh. Mwanri ameelezea umuhimu wa sekta ya viwanda kwa maendeleo ya kila mtanzania.
Mkuu wa Mkoa amewapongenza wanatabora hasa kupokea mabadiliko na kupunguza mimba za utotoni lengo likiwa ni kupata mhitimu wa Shahada ya kwanza kwa kila nyumba ya mkazi wa Tabora.
Aidha Mkuu wa Mkoa wa Tabora aliwahimiza wahitimu wote  kubuni namna ya  kujiajiri na kuwaajiri wengine, ili kuondokana na tatizo la ukosefu wa ajira linalolikumba Taifa letu na mataifa mengine duniani.
 Pia aliwahimiza wahitimu wote kukumbuka kurudisha mikopo waliyokopeshwa na Serikali ili kuongeza uwezo serikalini wa kukopesha wengine. Nendeni mkawe mabarozi wazuri wa chuo cha “AMUCATA”. Haya ni mahafari ya saba tangu Chuo Kianzishwe.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU