Askofu Dallu akemea uchumba sugu


Na Sr. Tuzo Nyoni OSB, Songea

WAamini wameaswa kuachana na tabia ya kuishi uchumba sugu bila kufunga ndoa. Badala yake wafunge ndoa ili wapate kupokea sakramenti mbalimbali katika kanisa.
Hayo yamesemwa hivi karibuni na Askofu Mkuu Damian Dallu wa jimbo Kuu Katoliki  Songea, wakati akihubiri katika Misa Takatifu ya jubilee ya miaka hamsini   ya Parokia ya Mtakatifu Martin wa Tur Mpandangindo iliyopo katika jimbo Kuu Katoliki Songea.
Askofu Dallu amesema kuwa, suala la uchumba sugu limekuwa likijitokeza katika parokia nyingi jimboni Songea na kuhimiza kuwa, waamini hawana budi kushika amri za Mungu na Kanisa kikamilifu.
Ameongeza kuwa, suala la kutoa zaka kwa waamini ni la msingi na kwamba waamini waachane na tabia ya kutoa zaka kwa Kanisa wakati wanapokuwa na majukumu ya kusimamia na kupokea sakramenti tu.
Akizungumzia sherehe ya Jubilei ya miaka 50 ya parokia hiyo ya Mpandangindo Askofu Dallu amesema , anatoa shukrani kwa uwepo wa wamisionari Wabenediktini walioleta Imani katika jimbo Kuu Katoliki Songea.
 Aidha amewataka waamini kuzisafisha nafsi na kuishi maisha yanayompendeza Mungu, na kuendelea kuliishi Neno la Mungu kama walivyofundisha wamisionari hao na kuwataka waamini kuwa na roho ya huruma, upendo na ukarimu kwa Kanisa zima la Mungu na kulitegemeza Kanisa.
Askofu Dallu amesema, Yesu Kristo tunakutana naye katika maisha ya kila siku na kufafanua kuwa  tunakutana na Yesu katika Misa Takatifu, katika Neno la Mungu, katika Ibada za kuabudu Ekaristi Takatifu.
Aidha katika mafundisho ya katekesi na katika matendo mema kwa wenzetu kama alivyofanya mtakatifu Martin wa Tur mlinzi wa parokia ya Mpandangindo ambaye alitoa hata kipande cha nguo yake kwa ajili ya wahitaji.
Parokia ya Mpandangindo kwa sasa inahudumiwa na mapadri wamisionari wa shirika la Wakarmel ambao hapa nchini Tanzania wapo katika Jimbo Katoliki  Morogoro  wapo parokia ya Malolo na Kihonda-, wapo pia Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam katika parokia ya mtakatifu Peter Claver Mbezi Luise, Parokia ya Teresia Mtoto Yesu Mbezi Mwisho na parokia ya Malamba ya Yohane wa Msalaba.
 Jimbo Kuu Katoliki Mbeya wapo katika parokia ya Yakobo Mtume  Uyole, na katika Jimbo Kuu Katoliki Songea Parokia ya Mpandangindo  ya Mtakatifu Martin wa Tur.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU