Mbunge kuanzisha chama cha Moyo Mtakatifu wa Yesu bungeni

 Rodrick Minja na Ndahani Lugunya, Dodoma

MBUNGE wa Rombo, Joseph Selasini amesema ataanzisha tawi la chama cha kitume cha Moyo Mtakatifu wa Yesu katika Jumuiya yake iliyopo Bungeni huku akimwomba Askofu Mkuu wa Jimbo Katoliki  Dodoma, Mhashamu Beatus Kinyaiya kuwa tayari kufanya uzinduzi pindi atakapoanzisha chama hicho cha Kitume.
Amesema hayo katika kilele cha Jubilei ya Miaka 100 ya Chama cha Kitume cha  Moyo Mtakatifu wa Yesu kiliyofanyika katika viwanja vya Hija Mbwanga Jimbo Kuu Katoliki Dodoma.
Wakati huo huo, Spika Mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mama Anna Makinda  ameongoza harambee kwa ajili ya ujenzi wa jengo la Groto ya sanamu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu na kufanikiwa kukusanya TSh 8,493,750.
Mbunge Selasini ametoa ahadi hiyo alipopata nafasi ya kuzungumza akiwa miongoni mwa wanachama wapya 75 walipokelewa kwenye Chama cha Kitume cha Moyo Mtakatifu wa Yesu kwenye kilele cha jubilei hiyo.
Selasini amemshukuru Spika Staafu Makinda kwa jitihada zake za kueneza na kukoleza imani ya Kanisa tangu alipokuwa bungeni alipowakusanya wabunge Wakatoliki na kuanzisha jumuiya ndogondogo, ambapo na yeye alibahatika kuwa mwenyekiti wa jumuiya hiyo bungeni.
Katika salamu zake, Selasini amesema Wanamoyo Mtakatifu wa Yesu wanapoadhimisha Jubilei ya Miaka 100 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1919 nchini, wasisahau jukumu kubwa walilonalo la kukeneza chama hicho kila mahali.
“Nami naomba niungane na mwenzangu (Makinda) kuwakumbusha kuwa, leo hii tunapoadhimisha jubilee hii ya miaka 100 tangu chama kianzishwe nchini, tusisahau kuwa jukumu kubwa tulilo nalo kwa sasa ni kueneza chama hiki kila mahali,” amesema Selasini.
Akizungumza katika harambee hiyo Askofu Mkuu Kinyaiya amesema ni jambo zuri waliloliwaza viongozi wa Taifa wa kuenzi Moyo Mtakatifu kwa kujenga groto hiyo ya Sanamu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu sanjari na kufanyia kilele cha maadhimisho hayo Jimboni Dodoma.
Amesema umefika wakati Wakristo kujiunga na chama cha kitume cha Moyo Mtakatifu wa Yesu kwani wao ni chumvi na mwanga kwa wengine hususani katika kukuza imani.
Askofu Kinyaiya amezungumzia pia suala la watoto wa mitaani akisema kuwa kila mmoja  akiwajibika katika nafasi yake tatizo la watoto wa mitaani litapunga na hata siyo kupungua litatokomea kabisa katika mikoa na majimbo yetu.
“Upendo umekuwa ukitoweka kila siku ndani ya familia zetu, ugomvi, mafarakano, mapigano, uhasama, chuki, fitina vyote hivi vinasababisha hata watoto wetu wazikimbie familia na makazi yao ya nyumbani na kukimbilia kuja kuishi mitaani ambako wanazidi kuharibika zaidi kwani wanakosa hata malezi ya wazazi,” amesema
Akaongeza: “Hakikisheni kuwa mnakuwa watu wa kufundisha na kurekebisha tabia za watoto na vijana wenu ili wabadilike kwani wakibadilika hata magerezani kutakuwa hakuna wahalifu na ni mategemeo yangu kuwa siku moja magereza yote yanakuwa hayana wahalifu ili tuyabadili yawe ni madarasa kwa ajili ya watu kusomea.”
 Askofu Kinyaiya  amesema wakati mwingine Wanamoyo na Wakatoliki wamekuwa waoga wa kushauri wanapomuona mtu anafanya au kuelekea kufanya vibaya kwa kumuonea aibu jambo ambalo siyo sahihi.
“Usimuonee aibu mwambie, mpashe tu na ndiyo maana Moyo Mtakatifu wa Yesu umefunguliwa pale, mlango umefunguliwa na sisi tumepata nguvu hiyo tuitumie tuifanyie kazi,” amesema.
Akizungumzia suala la ndoa amesema kuwa, upendo wa kweli unahitaji sadaka, hivyo amewataka wanandoa hususani vijana kulitambua hilo, kwani kundi lao ndilo linaloongoza na kuathiriwa kwa kukosa upendo na kuvumiliana.
“Sasa ndugu zangu na hasa nyie vijana wale walio na hizi ndoa freshi freshi hilo kwao ni taabu kweli, wakikoseana kidogo toka hapa kwenda kwa mama yako!” ameeleza.
Awali akizungumza juu ya ujenzi wa groto hiyo, Mwenyekiti wa Kitaifa wa Chama cha Moyo Mtakatifu wa Yesu, Longinius Kagaruki amesema itagharimu Sh 7,000,000 lakini kwa kuwa tayari ipo pia groto ya Mama Maria pembeni ya watakapojenga groto ya sanamu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu itabidi iboreshwe kwa kuwekewa mazingira mazuri kwa ajili ya watu kusali kwa utulivu zaidi.
“Kwa kweli groto ya Mama Maria imejengwa vizuri, ila mazingira ya watu kukaa na kusali hayapo vizuri, hivyo tumeona ni bora tuyaboreshe ili watu waweze kusali kwa utulivu na kwa kutafakari kwa kina sala na maombi wanayokuwa nayo,” amesema Kagaruki.
“Groto ya sanamu ya Moyo Mtakatifu wa Yesu itagharimu kiasi cha shilingi milioni saba tu na shilingi milioni tatu nyingine ndizo zitatumika kuboresha mazingira ya groto ya Mama Maria,” amesema.
Kwa mujibu wa Kagaruki, tayari Askofu Mkuu Kinyaiya ameshawapa eneo na kuwaonesha mahali ambapo watajenga groto hiyo  itakayokuwa ni alama ya miaka 100 ya chama hicho tangu kianzishwe.
Viongozi hao wamesema sanamu itakayowekwa kwenye groto hiyo imenunuliwa Sh milioni 2 kutoka katika duka kubwa la visakramenti la
Jimbo Kuu Katoliki Dodoma lililopo katika Parokia ya Mtakatifu Petro Swaswa.
 Spika Mstaafu wa Bunge la Jamhuri ya Mungano wa Tanzania, Anna Makinda, amewashauri Wanamoyo Mtakatifu wa Yesu nchini, kushuka hadi ngazi ya Jumuiya Ndogondogo za Kikristo kueneza chama hicho.
Mama Makinda ametoa ushauri huo wakati akitoa salamu kwa wanachama wa Moyo Mtakatifu wa Yesu, baada ya Ibada ya Misa Takatifu ya Kilele cha Jubilei ya Miaka 100 ya chama hicho kitaifa, iliyofanyika jimboni Dodoma.
Makinda ambaye pia ni mwanachama wa chama hicho cha kitume, amesema ipo haja kwa wanachama hao wa Moyo Mtakatifu wa Yesu kujizatiti katika kukieneza chama hadi ngazi ya chini ya Kanisa hususani jumuiya Ndogondogo za kikristo, ili waamini mahalia watambue umuhimu wa kufanya ibada na kutoa heshima kwa Moyo Mtakatifu wa Yesu.
Amesema wao kama wanachama wanapopeleka ujumbe katika jumuiya, baadhi ya waamini hasa vijana hushangaa kukiona na kukisikia chama hicho, akitolea mfano katika Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam anakotoka yeye.
“Naomba nitumie nafasi hii pia kuwashauri wanachama wenzangu wa Moyo Mtakatifu wa Yesu mliopo hapa, twendeni tukakieneze chama hiki hadi kwenye jumuiya ndogondogo za Kikristo ili watu watambue na kujua umuhimu wake ni nini,” amesema.


Comments

  1. Moyo Mtakatifu wa Yesu... Ufalme wako ufike...
    Hongera sana Mhe. Mbunge Joseph Selasini. Moyo huo ukawe chachu kwa wengine wengi ili wavutiwe na moyo Mtakatifu wa Yesu na kujiunga kwa wingi katika utume huo ili kueneza ibada na kuuhesgimu moyo Mtakatifu wa Yesu uliojaa mapendo kwetu wanadamu. Wote tunaalikwa kuukimbilia na kuutuliza moyo Mtakatifu wa Yesu.

    ReplyDelete

Post a Comment

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU