Askofu Banzi aadhimisha jubilei miaka 25 ya Uaskofu

  Na Domonic Maro- Tanga.
ASkofu wa Jimbo Katoliki Tanga Mhashamu Anthony Banzi ameadhimisha jubilei ya fedha (miaka 25) ya uaskofu.
Maadhimisho ya Jubilei hiyo yamefanyika hivi karibuni katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Anthony wa Padua Chumbageni Jimboni humo.
Papa Fransisko amemtumia Salamu za pongezi Askofu Banzi akisema anamshukuru Mungu kwa kulitumikia Kanisa katika Jimbo Katoliki Tanga.
Akisoma salamu hizo kwa niaba ya Baba Mtakatu, Balozi wa Baba Mtakatifu Nchini Askofu Mkuu Marek Solczyn’sk amesema kuwa, Papa anampongeza Askofu Banzi kwa utume uliotukuka katika Kanisa la Tanzania na hasa Jimbo la Tanga. Anamuombea baraka za Mungu aendelee kuchunga kondoo wa Mungu na kulikuza Kanisa jimboni Tanga.
Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania TEC limempongeza Askofu Banzi kwa utume uliotukuka huku likimuombea na kumshukuru kwa kujitoa kwa moyo bila kuchoka kwa muda wa miaka 25 ya uaskofu wake.
Akiwakilisha salamu hizo  za TEC Makamu Mwenyekiti wa TEC Askofu Flavian Kassala amesema kuwa,  Baraza linamshukuru Mungu kwa zawadi ya Askofu Banzi katika Kanisa la Tanzania.
Pia linamshukuru Askofu Banzi kwa kuitikia wito  wa Upadri hatimaye  uaskofu.
Amesema kuwa, Askofu huyo amejitoa kuwadumia masikini  na watanzania bila kuchoka zaidi wanamuombea afya njema aendelee kumtumikia Mungu kwa sadaka zake.
“Baraza la Maaskofu linatambua kuwa safari ya kichungaji kwa muda wa miaka 25 siyo rahisi hata kidogo kwani umepitia vipindi vyote ya uchungu na furaha.
Hivyo  Baraza linakushukuru kwa kuweza kujitoa na kutumika bila kuchoka, kufanya kazi ndani ya baraza na hata nje ya Taifa kwa lengo la kumuhubiri Kristo.
Tunakuombea  kwa Mungu aendelee kukushika mkono katika safari nyingine ya kulitumikia Kanisa kwa miaka mingine  zaidi ili uweze kulihudumia Kanisa la Tanzania, Afrika na zaidi sana dunia yote,” amesema Askofu Kassala kwa niaba ya Kanisa Katoliki Tanzania.
Aidha ameishukuru Serikali kwa kushirikiana na Kanisa katika kuihudumia jamii.
Amesema kuwa Kanisa  linatambua mchango wa Serikali ya Jamuhuri ya Muungano wa Tanzania  inavyoendelea kutoa ushirikiano na Kanisa Katoliki huku ikiendelea kulinda Uhuru wa kuabudu.
Pia Linatambua jitihada za Rais  John Pombe Magufuli kwa kushirikiana na Kanisa Katoliki katika masuala mbalimbali bila kuchoka.
“Zaidi sana leo tunamshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mh. John Magufuli kwa kujitoa kumuhudumia  Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki  Dar es salaam Askofu Mkuu  Jude Thaddaeus Ruwa’ichi tangu alipokuwa mgonjwa kule KCMC hadi aliposafirishwa kwenda Hospitali ya Tiba ya Mifupa MOI akapatiwa matibabu na sasa hali yake inaendelea kuimarika.
Tunamshukuru sana kwa majitoleo hayo na tunakuomba Mh. Ummy Mwalimu upeleke salamu na shukrani zetu kwa Rais kwani tumefarijiwa na ushirikiano wake huo,” amesema.
Amehitimisha kwa kusema kwa ushirikiano wa serikali na Kanisa Katoliki utaendelea kulinda tunu ya  haki za binadamu kwani kulinda tunu hizo hakuna utengano wa itikadi za dini, kabila au vyama vya siasa bali ni wajibu wa wote.
 Askofu Mkuu Mstaafu wa Jimbo Kuu Katoliki Dar es Salaam, Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo amempongeza Mhashamu Banzi kwa kuadhimidha Jubilei ya Miaka 25 ya Uaskofu wake Septemba 15, mwaka huu na kumtaka asikate tamaa kwa mazingira magumu na changamoto alizopitia na atakazopitia kwani ni sehemu ya maisha ya uchungaji.
Kadinali Pengo amesema licha ya mafanikio katika utume wake, pia zimekuwepo kauli na changamoto mbalimbali zilikaribia kumkatisha tamaa, lakini Mungu ameendelea kuwa pamoja naye katika safari ya kuliongoza kundi lake.
Amemkumbusha Askofu Banzi kuwa, miaka 25 ya uaskofu haipaswi kuwa kituo cha kupumzika, bali kiwe mwanzo mpya wa kuendelea na safari yake ya kiimani hadi Mungu atakapomuita hivyo, aendelee kumuomba Mungu amjalie afya na kuliombea Jimbo la Tanga na Kanisa kwa ujumla.
Kwa upande wake, Askofu Banzi amewashukuru viongozi wa serikali, maaskofu, mapadri, watawa wa kike na wa kiume, waamini na watu wote wenye mapenzi mema kwa kushirikiana naye kwa kila hatua ya maisha yake zaidi sana katika miaka ya 25 ya uaskofu wake.
Amesema kuwa, anafurahia wito wake kama Askofu na hata angeambiwa aanze leo kuchagua wito wa maisha yake, wito wake ni upadri.
“Ninapenda wito wangu na ninamshukuru Mungu kwa ulinzi wake hadi kufikia hapa. Ninawashukuru wazazi wangu, ndugu jamaa na marifiki kwa kunilea na kuniingiza katika imani hii.
Ninawashukuru wanadarasa wote kuanzia shule za msingi, sekondari, seminarini na mapadri wote kwa ushirikiano hadi nimefikia siku hii.
Zaidi sana niwashukuru Maaskofu wenzangu kwa ushirikiano wa dhati kuanzia ngazi ya Baraza kwani kupitia sala zenu na ushirikiano nimeweza kufika hapa,” amesema Askofu Banzi.
Amemshukuru Rais wa Jamhuri  ya Muungano wa Tanzania  John Pombe Magufuli jinsi anavyo pambana na ufisadi na kufunga mianya ya rushwa na kuendelea kuboresha huduma mbalimbali za kijamii na kufungua njia za kiuchumi.
“Tunashuhudia  miradi mbalimbali  ya maendeleo ya kiuchumi ukiwemo ujenzi wa reli ya kisasa ya Standard Gauge, miradi mikubwa ya umeme na mradi wa bomba la mafuta kutoka nchini Uganda hadi Tanga, kuboresha usafiri wa anga kwa kununua ndege za kisasa na kuboresha miundombinu ya barabara na huduma nyingine za maendeleo ya kijamii.
Kwa hayo yote yanayotekelezwa na serikali, si kwamba  Kanisa Katoliki Tanzania na Jimbo Katoliki Tanga tunakuwa  watazamaji tu, la hasha! Tunashiriki kikamilifu kuibua na  kuinua yale ambayo yanahitajika kwa watanzania wote kwani Viongozi wa Kanisa wana wajibu wao kiroho na kimwili,” amesema Askofu Banzi.
Waamini mbalimbali wa Jimbo Katoliki Tanga wamesema kuwa, Askofu Banzi katika miaka yake 25 ya kuliongoza Jimbo Katoliki Tanga, kumekuwa na kukua kwa imani hasa kwa waamini kupokea na kuishi sakramenti mbalimbali.
Mengine wanayofurahia wamesema ni ongezeko la vituo vya afya, ukuaji wa miito mbalimbali, ongezeko la mashirika ya kitawa ya kike na kiume, kuboresha na kukuza sekta ya elimu kwa kuanzisha shule za chekechea, sekondari na vyuo mbalimbali.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU