Maaskofu wataka mapadri kutoa mahuribi hai si vijembe

Na Padri Anthony Chilumba
RAis wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania ambaye pia ni Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu  Katoliki Mbeya,Mhashamu Gervas Nyaisonga amewataka Wahubiri wa  Neno la Mungu kuzingatia kanuni bora za utoaji mahubiri yao kwenye maadhimisho mbalimbali ya  Liturujia.
Ameyasema hayo wakati anafungua Warsha  ya Uboreshaji wa kutoa Homilia iliyofanyika kwenye Makao Makuu ya Baraza la Maaskofu Katoliki  Tanzania iliyowakutanisha wajumbe wapatao 60 toka majimbo 26, wakiwemo Manaibu wa Maaskofu kutoka majimbo 15.
Askofu  Nyaisonga amewaambia washiriki hao kuwa, waamini wanaguswa sana na mahubiri yanayotolewa kanisani,hivyo ingawaje ni ya muda mfupi yanahitajika sana ili kuwatia moyo wakristo wanaoyasikiliza.
Kwa mujibu wa Askofu Nyaisonga Ibada mbalimbali zinazoongozwa na mapadri zinapaswa kuwa hai na kwamba uhai huo unachangiwa na mahubiri ya adhimisho husika.
“Mahubiri yenu yasidorore wala yasikinaishe wasikilizaji kwa sababu yakiwa hivyo hayatakidhi lengo la Uinjilishaji,” amesisitiza Mhashamu Nyaisonga.
Katika kufikia malengo hayo amewahimiza Mapadri hao wakiwemo Waratibu wa Liturujia  pamoja na Wakurugenzi wa Uchungaji Majimboni, kujiandaa vizuri kwa  kusoma machapisho mbalimbali na kuzingatia sala wakati wa kuandaa mahubiri yao.
Mapema akizungumza kwa niaba ya Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania TEC, Naibu Katibu Mkuu WA TEC Padri Daniel Duwe amewakaribisha washiriki wote katika Makao Makuu ya Baraza na kuongeza kuwa fursa ya Warsha hiyo itaboresha mawasiliano baina ya Baraza na Majimbo kwa kuwa inawakutanisha Viongozi wa Kanisa ambao hukutanika kwa nadra sana.
Kwa upande wao Katibu Mtendaji wa Idara Padri Paul Chiwangu na Askofu Mwenyekiti wa Idara ya Liturujia,Mhashamu Askofu Salutaris Libena waliwakaribisha wajumbe waliohudhuria Warsha hiyo ambayo iliongozwa na mada zilizotolewa na Askofu Msaidizi wa Jimbo Katoliki Bukoba Mhashamu Method Kilaini na Askofu Libena wa Jimbo Katoliki Ifakara amabye ni Mwenyekiti wa Idara ya Liturujia katika Baraza.
Mada ya kwanza ilitolewa na Askofu Libena ambaye alizungumzia juu ya Homilia, tafsiri ya Liturujia kadiri ya Hati ya Mtaguso wa Pili wa Vatikano pamoja na nafasi ya Liturujia katika maadhimisho ya fumbo la Ekaristi.
Wakiwa wanashirikishwa kazi za Kikuhani za Kristo,wahubiri wanapaswa kufuata nyayo za Kristo aliyelihubiri Neno la Mungu pale aliposema: “Tubuni na kuamini na kwamba Ufalme wa Mungu umekaribia.”
Katika hali hiyo mapadri hawana budi kulipatia heshima na uzito wa pekee Neno la Mungu kwa sababu Yesu yumo ndani mwake.
Ukiondoa uwepo wa Kristo katika Neno, yumo pia katika Ekaristi na katika Sakramenti zote.
Kristo yupo pia katika watumishi wake sanjari na kwenye jumuiya kutokana na kauli yake aliyosema: “Wakutanikapo wawili au watatu kwa jina lake, yeye yupo katikati yao.”
 Amehitimisha mada yake kwa kuwakumbusha washiriki lengo la kila  adhimisho la Kiliturujia;yaani Mungu anatukuzwa na wanadamu wanapata wokovu wao.
Mada ya pili ilitolewa na Mhashamu Askofu Kilaini ambaye alijikita kuzungumzia  juu ya Mwongozo wa Mahubiri katika adhimisho la Kiliturujia.
Alieleza kuwa msingi wa huduma hiyo ni Yesu mwenyewe aliyewaagiza mitume wake na waandamizi wao: “Basi enendeni mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi, mkiwabatiza kwa jina la Baba na Mwana na Roho Mtakatifu na kuwafundisha kuyashika yote niliyowaamuru ninyi”(Mt.28:19-20).
Katika kuzingatia hilo ndio maana hata Papa Fransisko katika barua yake ya Kichungaji  aliyoiita “Evangelii Gaudium” anasema kuhubiri ni mojawapo ya vipaumbele katika maisha ya Kanisa.
Kwa muhtasari Papa huyo amesisitiza umuhimu wa kila Mhubiri kujiandaa ipasavyo kabla hajapanda mimbarini kuhubiri.
Kwa mujibu wa Kiongozi huyo wa Wakatoliki duniani Mhubiri asiyesali na kujiandaa kwa ajili ya mahubiri yake si makini na hawajibiki na amemwita nabii mwongo.
Askofu Kilaini aliwakumbusha wahubiri wote kuzingatia hatua muhimu zinazotakiwa kufuatwa wakati wa kuandaa mahubiri na wakati wa kuhubiri kwenyewe.
Aidha,mahubiri yajengwe katika Neno la Mungu na si vinginevyo.
Aliwaasa kutotumia mimbari kwa kujihubiria wenyewe kwa majigambo mbalimbali au kuwakemea wakristo bila sababu za msingi.
Pia mhubiri asitumie muda wa mahubiri kwa kutoa utetezi dhidi ya tuhuma zake(zikiwepo),kuwasema watu,vijembe au kila Dominika kurudia neno lile lile alilolisema siku za nyuma.
Alihitimisha mada yake kwa kuwakumbusha wanawarsha kuwa mahubiri ni sehemu ya Liturujia na ni Ibada.
Mahubiri yaguse mahitaji ya wasikilizaji kusudi yamjenge kiroho na kimwili na hatimaye achukue hatua.
Kwa kuwa mahubiri ni sehemu ya Ibada inahimizwa,sehemu hiyo iongozwe na  Hiarakia na kama Mlei ana jambo la kuwaambia wakristo wenzake litafutiwe nafasi nyingine badala ya kipindi cha mahubiri.
Baada ya maswali na majibu mbalimbali yaliyohusu Liturujia,yalitolewa Maazimio mbalimbali kutokana na mada zilizozungumziwa.
Kisha Askofu Libena aliwashukuru wajumbe toka majimbo yaliyohudhuria warsha hiyo ya aina yake na kwa namna ya pekee alimshukuru Katibu Mkuu wa Baraza aliyetafuta fedha kwa ajili ya mafunzo hayo.
Kabla hajamaliza shukrani zake alimpongeza na kumshukuru Mhashamu Askofu Kilaini kwa utayari wake wa kuja kutoa mada kwenye mkusanyiko huo uliowakutanisha Manaibu wa maaskofu, wakurugenzi wa uchungaji na waratibu wa Liturujia majimboni.
Majimbo yote Katoliki yalituma wajumbe isipokuwa majimbo ya Bukoba, Geita, Ifakara, Kondoa, Mahenge, Mpanda, Singida na Sumbawanga.
Kabla hajatoa Baraka za kufungia warsha Askofu Mwenyekiti alitangaza kifo cha Padri wa Jimbo la Ifakara Castor Mkapila(63) aliyefariki kwenye Hospitali ya Rufaa ya Mtakatifu Fransisko, Ifakara, tarehe 18 Septemba mwaka huu.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU