‘Tutapata kila kitu kupitia Maria’ Katibu Mkuu TEC


Na Pascal Mwanache

WAAMINI nchini wameaswa kusali, kujikabidhi na kujiweka wakfu kwa moyo Imakulata wa Bikira Maria kama njia pekee ya kutafuta amani ya mtu binafsi, familia, jumuiya, Kanisa na Taifa.
Rai hiyo imetolewa na Katibu Mkuu wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Padri Raymond Saba katika homilia aliyoitoa wakati wa adhimisho la kilele cha Yubilei ya miaka 100 tangu Bikira Maria alipowatokea watoto wa Fatima, Lucia, Fransisko na Yasinta, adhimisho lililofanyika katika Parokia ya Msimbazi, Jimbo Kuu Katoliki Dar es salaam.
Padri Saba amesema kuwa ikiwa Mungu alimuona Maria kuwa njia ya kuwafikia wanadamu ulimwenguni, kwa nini wanadamu wasimtambue na kujikabidhi kwake ili awapeleke mbinguni, huku akiwataka waamini kutoona aibu kusali sala ya Rozari Takatifu.
“Salini rozari kwa kuwa ni chombo kitakacholeta amani duniani. Tusali rozari kila siku amani itarudi duniani, amani inayoanzia kwenye nafsi zetu. Kama malaika alitoka mbinguni akasema ‘Salamu Maria’ kwa nini mimi na wewe tuone aibu kusali” amehoji Padri Saba.
Aidha ameeleza kuwa moja ya maagizo ya Bikira Maria alipowatokea watoto wa Fatima aliwataka kufanya malipizi kwa ajili ya dhambi za dunia, hivyo ametumia fursa hiyo kuwakumbusha waamini kuwa tayari kujitoa sadaka kwa ajili ya wadhambi na kuziombea roho nyingi zinazoenda motoni kwa kukosa waombezi.
Amewaasa waamini kuwa imara katika imani kwa kuwa watu wengi wanaacha ukatoliki na kwenda kuhangaika kwenye madhehebu mengine wakitafuta uponyaji, huku akisema kuwa teolojia ya mateso na msalaba imepoteza maana yake kwa waamini wengi.
“Bikira Maria aliwataka watoto wale wafanye malipizi pale alipowauliza. ‘Je mpo tayari kujitoa ili mpate mateso ya kila aina kwa ajili ya kulipia dhambi zenu na ulimwengu na moyo Imakulata unaodhalilishwa?’ Watoto hawa wadogo kabisa walikubali. Kwetu sisi teolojia ya msalaba hatuipendi hata sisi wakatoliki. Ndiyo maana tunaacha ukatoliki kwa kutafuta uponyaji. Tungependa kuwa na Pasaka bila Ijumaa Kuu,” ameeleza Padri Saba.
Kwa nini Mama Maria atokee duniani tena 1917?
Akielezea nia ya kufanya Yubilei hiyo Padri Saba amesema kuwa waamini wanaalikwa kumrudishia Mungu shukrani kwa kuwapatia Bikira Maria ambaye haoni fahari tu kukaa mbinguni wakati huku duniani mambo hayaendi sawa, na hivyo anashuka kuwasaidia waamini wafuate njia iendayo kwa Mungu.
Pia ameeleza kuwa mwaka 1917 ambao Mama Maria alitokea huko Fatima, ni mwaka wenye sifa ya pekee katika historia ya ulimwengu, ambapo ni katika mwaka huo waprotestanti waliadhimisha miaka 400 tangu Martin Luther alipoanzisha uprotestanti uliosisitiza kuwa imani peke yake inatosha.
“Bikira Maria anapotokea anaagiza watu wasali, wafunge, wafanye toba na hija, na hivi anathibitisha kinachosemwa na Yakobo kwamba imani bila matendo ni bure. Lakini pia mwaka 1917 ndipo Freemasons walikua wanaadhimisha miaka 200 tangu waanze shughuli zao huko London Uingereza,” amesema.
Aidha ameongeza kuwa mwaka 1917 ndipo mapinduzi ya Urusi yalifanyika na hapo ukomunisti ukashika hatamu na kuteketeza imani ya kikristo, hapo ndipo makanisa yakavunjwa, mapadri na maaskofu wakafungwa. Pia amebainisha kuwa, mwaka 1917 ndipo Taifa la Marekani lilipoingia katika vita kuu ya kwanza ya dunia, na kushuhudia mvutano mkali baina ya Urusi na Marekani.
“Ni katika mazingira haya ndipo Bikira Maria anakuja na kutoa ujumbe kwamba watu wasali ili amani irudi duniani,” ameongeza.


Comments

Popular posts from this blog

SALA YA ASUBUHI:SALI HIVI..

Ujio wa Wamisionari wa Kwanza Tanzania Bara (2)

HISTORIA YA SHEREHE YA MOYO MTAKATIFU WA YESU