‘Kanisa siyo mshindani, ni mtumishi’ Ask. Ngalalekumtwa
RAIS wa Baraza la Maaskofu Katoliki Tanzania Mhashamu Tarcisius Ngalalekumtwa amesema kuwa Kanisa halina wazo lolote la ushindani katika utoaji wa huduma zake, bali linafanya hayo yote kwa kuwa huo ni utume na wito wake. Ameeleza hayo katika maadhimisho ya jubilei ya miaka 25 ya Tume ya Kikristo ya Huduma za Jamii nchini (CSSC), yaliyofanyika jijini Dar es salaam, na kubainisha kuwa Kanisa linatumia rasilimali zake kwa ajili ya ustawi wa taifa na watu wake. “Kanisa siyo mfanya biashara, na siyo mshindani ila ni mtumishi. Kanisa linaendelea kutoa huduma bora ikiwemo elimu bora na siyo bora elimu, afya na kuwatunza wenye dhiki. Hatuna nia ya kuingia ushindani, tunatumia rasilimali zetu kwa ajili ya taifa letu ili liwe lenye heshima, utu na ustawi” ameeleza Askofu Ngalalekumtwa ambaye pia ni Makamu wa Rais wa CSSC. Kauli hiyo imeungwa mkono na Rais wa CSSC Askofu Alex Malasusa aliyeweka wazi kwamba makanisa hayatoi huduma za afya na elimu kwa ajili ya kupata faida kiuchumi. Amese...